24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Ukawa wamwonya JK

Pg 1 ukawaNa Fredy Azzah, Zanzibar

UMOJA wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wamemuonya Rais Jakaya Kikwete, wakisema ndiye mwenye dhamana ya kulinda usalama wa wananchi na akiendelea kutumia vibaya vyombo vya dola, Novemba mwaka huu watamburuza Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) iliyopo The Hague, Uholanzi.

Kauli hiyo ilitolewa jana mjini Zanzibar na viongozi wa Ukawa, katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Kibanda Maiti wenye lengo la kutafuta wadhamini kwa mgombea urais wa umoja huo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa.

Akizungumza katika mkutano huo jana mjini hapa Katibu Mkuu wa CUF ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalimu Seif Sharif Hamad, alisema CCM wanahubiri amani wakiwa majukwaani lakini wakishuka wao ndio wa kwanza kuivunja.

“Kama kuna watu wana nidhamu ni watu wa Ukawa, Mbeya, Arusha, watu wawalikuwa wanasubiri kwa amani, polisi wanapiga mabomu, wao ndiyo wanaleta tensheni katika nchi, siyo wafuasi wa Ukawa.

“Namwambia Kikwete (Rais), atimize wajibu wake, akifanya vinginevyo watakwenda ICC, Kikwete ondoka kwenye nchi ikiwa salama kama ulivyokabidhiwa ikiwa salama, wananchi wakukumbuke kuwa umeiacha salama,” alisema Maalim Seif ambaye pia ni mgombea urais wa Zanzibar kupitia umoja huo.

Mbatia

Akihutubia katika mkutano huo, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, amewataka wanasheria wa Ukawa, kuanza kuandika matukio yote yanayotokea nchini kwa sasa ili wayawasilishe katika Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Uhalifu (ICC).

“Tumeshawaagiza mawakili wetu waandike matendo yote maovu yanayofanywa, waandikie ICC, wapeleke nakala kwa mabalozi wote ili Fatou Bensouda (Mwendesha mashitaka Mkuu wa ICC) aje aanze kuangalia yanayofanyika hapa.

“Tumechoka kudanganywa, tumechoka kuibiwa ushindi wetu, mwaka huu tunasema, hapana, hapana. Walikuja kuandikisha  watu wao hapa na baada ya Ukawa kutangaza mgombea  watu wao wote sasa wamehamia Ukawa,” alisema Mbatia.

Alisema Watanzania kwa sasa wanataka mabadiliko kwa asilimia 99, na jeshi la polisi likiendelea kuvunja amani, Novemba mwaka huu watakwenda ICC.

Juma Duni

Naye Mgombea Mwenza wa Chadema, Juma Duni Haji, alisema ni bahati mbaya sana watawala wanadhani kutumia mabavu kutawasaidia kubaki madarakani  jambo  ambalo kwa sasa haliwezi kutokea.

Lowassa na Kingunge

Kwa upande wake Lowassa alisema kitendo cha CCM kumvua wadhifa wake Kamanda wa UVCCM, Kingunge Ngombale Mwiru kwa sababu tu mwanasiasa huyo mkongwe alitumia demokrasia kueleza hisia zake ni kuchuma laana.

Alisema Kingunge ambaye ni mmoja wa waasisi wa TANU na CCM, alikuwa amebaki kama mfano ndani ya chama hicho kutokana na historia yake.

“Nianze kwa kueleza masikitiko yangu kwa hatua aliyochukuliwa mzee Kingune jana (juzi), mzee huyu alibaki kama kielelezo cha TANU, yote yaliyomfika ni kutokana na kutoa maoni yake, hatua waliyochukua ni laana… laana ya Kingunge itawapata,” alisema Lowassa.

Lowassa alisema amefika Zanzibar kuomba wadhamini kwa sababu anataka kupambana na umaskini na anauchukia.

“Nilivyoona sipewi nafasi ya kupambana nao huko CCM nikaondoka, niliondoka kwa maneno ya Mwalimu Nyerere (Baba wa Taifa) kwamba Watanzania  wanataka mabadiliko, wasipoyatapa ndani ya CCM watayapata nje ya CCM, naifahamu Tanzania,” alisema Lowassa.

Akizungumzia kuhusu Katiba mpya, alisema tangu wakati wa G55 alikuwa ni muumini wa Serikali tatu na kwamba hata kwenye Tume ya Jaji Wairioba alisema hilo.

“Nilisema nataka Serikali tatu lakini Muungano ubaki, muungano huu siyo wa uongozi ni wa watu. Nataka Muungano imara ndani ya watu imara, Serikali tatu  inayozingatia mahitaji  ya watu sawa ya watu wa Zanzibar na wale wa Bara,” alisema.

Mgeja

Aliyekuwa mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja, alisema Ukawa ni meli iliyosalama na itawavusha Watanzania kwenda kwenye maisha yenye matumaini.

Alisema Watanzanai wanataka mabadiliko na ndiyo maana aliamua kuachana na chama chake cha awali ili awe sehemu ya ukombozi.

“Ndiyo maana nikaondoka CCM… tatizo la Chama Cha Mapinduzi ni mfumo ambao unatesa Watanzania. Tumejitahidi sana kuuguza mgonjwa, lakini ikifika mahali unauguza mgonjwa haponi ujue kuna tatizo kubwa,” alisema Mgeja.

Alisema moja ya matatizo makubwa ya chama chake cha awali ni watu kutotaka kuambiwa ukweli.

“Kingunge (mmoja wa waasisi wa CCM na TANU),  juzi kwa sababu ya kusema ukweli, wamemfukuza kwenye ukamanda wa UVCCM, Mzee Moyo (Hassan Nassor ), naye kwa kusema ukweli yakampata yaliyompata na mimi kwa kusimamia ukweli mwaka juzi kwa kutaka nafasi ya uenyekiti itenganishwe na urais wakataka kunichinja,” alisema.

Alisema licha ya kuwa Katiba ni moja  ya mahitaji makubwa ya wananchi, jambo hilo halijawahi kuwa ajenda ya CCM.

“Namuomba Kinana (Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman) atoe walau muhutasari wa lini CCM iliwahi kujadili suala la Katiba, lakini ilipoanza presha ya msukumo wa Katiba kutoka Chadema, CUF ilibidi Rais (Jakaya Kikwete) aufuate,” alisema.

Alisema baada ya Ukawa kuona mambo hayaendi, wakaamua kujitoa kwenye Bunge Maalumu la Katiba na aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samia Suluhu Hassan, amepewa zawadi kwa kuteuliwa kuwa mgombea mwenza wa CCM.

Mbowe

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo  (Chadema), Freeman Mbowe, alisema ni vema viongozi wakavitumia vyombo vya ulinzi na usalama kwa masilahi ya watu wote na siyo kwa chama kimoja.

“Tunavihakikishia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kuendelea kulinda wananchi kwa sababu hata tukiunda serikali yetu, hatutavipeleka likizo, vitaendelea na jukumu lake.

“Hawana sababu ya kuwa na hofu, wataingiwa hofu wanaounda vikundi vya kutesa Watanzania, tunawataka viongozi wetu watumie vizuri majeshi yetu, siyo mali yao, wasitumike kubagua wananchi siyo kulinda chama kimoja cha kisasa” alisema.

Alisema Zanzibar ni lulu ambayo dunia nzima inaitolea macho lakini Wazanzibari hawaioni kwa kuwa hawajafaidika.

“Zanzibar inajulikana kuliko hata Tanzania bara, ni lulu inayotakiwa na dunia nzima, lakini wananchi wengi wa Zanzibar hawajui thamani ya Zanzibar kwa sababu maisha yao hayafanani na thamani ya Zanzibar.

Umeme

Tokea saa 3.45 asubuhi umeme ulikatika katika mji mzima wa Unguja na kukwamisha shughuili kadhaa za uzalishaji mali huku watu kadhaa wakishindwa kufuatilia mkutano wa Ukawa hadi uliporejea majira ya saa 11.45 jioni hali iliyoibua hisia  na kueleza kukatika huko ni kutokana na sababu za kisiasa.

Katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Abeid Amani Karume mjini  Zanzibar, Lowassa alipokewa na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, Mjumbe wa Braza Kuu la CUF Jussa Ladhu, Waziri wa zamani wa SMZ Mansoor Yussuf Himid na msafara wake kupita katika barabara kuu ya Nyerere hadi eneo  la mkutano.

Majimbo Ukawa hadharani

Vyama vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi (Ukawa) vimetoa orodha ya mgawanyo wa majimbo 203 ya Ubunge Tanzania bara.

Katika mgawanyo huo,  Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema) kitasimamisha wagombea katika majimbo 137 kikifuatiwa na Chama cha Wananchi(CUF) majimbo 49, NCCR Mageuzi 14 na NLD ikiambulia majimbo matatu huku majadiliano yakiendelea katika majimbo 12.

Katika mgawanyo huo, Chadema imechukua majimbo yote ya mikoa ya Arusha, Mara, Shinyanga, Geita, Njombe, Rukwa, Manyara, Katavi na Singida huku CUF ikichukua majimbo yote ya Mkoa  wa Lindi.

Wakati NCCR Mageuzi ikijipatia majimbo sita ya Mkoa wa Kigoma, Chadema wataweka mgombea katika majimbo ya Kigoma Kaskazini na Kigoma Mjini.

Chama cha NLD kinachoongozwa na Dk. Emanuel Makaidi kimepata majimbo matatu ya Lulindi, Masasi na Ndanda katika mkoa wa Mtwara kikigawana na CUF majimbo yaliyobaki.

Katika Mkoa wa Simiyu, CUF imeambulia Jimbo la Busega huku majimbo mengine yakichukuliwa na Chadema.

Katika Mkoa wa Dodoma, majimbo ya Mtera na Kibakwe yameenda  NCCR Mageuzi huku Kongwa, Bahi, Chilonwa na Dodoma Mjini yakienda Chadema na yaliyobaki yatakuwa ya CUF.

Katika Mkoa Kagera, Jimbo la Bukoba Mjini limechukuliwa na Chadema, Vijijini CUF, Nkenge na Ngara yakienda NCCR Mageuzi na yaliyobaki yamechuliwa na Chadema.

Mkoa wa Mbeya, majimbo 11 yamechukuliwa na Chadema huku NCCR Mageuzi ikipata jimbo moja la Ileje.

Katika Mkoa wa Dar es Salaam, majimbo matano ya Ubungo, Kawe, Ukonga, Ilala, na Kibamba yamechukuliwa na Chadema, huku CUF ikisimamisha wagombea katika majimbo matatu ya Kinondoni, Temeke na Mbagala. Majimbo mawili ya Segerea na Kigamboni yakiendelea na mashauriano.

Mkoani Iringa, Chadema imechukua majimbo yote kasoro Jimbo la Mufindi Kusini lililochukuliwa na NCCR Mageuzi.

Katika Mkoa wa Tabora, majimbo sita ya Nzega Mjini, Igunga, Urambo, Ulyankulu, Sikonge na Manonga yamekwenda Chadema huku mengine sita yaliyobaki yakichukuliwa na CUF.

Majimbo nane ya Mkoa wa Tanga yamechukuliwa na CUF huku manne ya Kilindi, Muheza Korogwe na Korogwe Mjini yakienda Chadema.

Mkoani Morogoro, Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki na Kilosa yamechukuliwa na CUF na yaliyobaki yote yamekwenda Chadema.

Katika Mkoa wa Pwani, majimbo matatu ya Chalinze, Kibaha Mjini na Vijijini yameenda Chadema na yaliyobaki yamekwenda kwa CUF.

Mkoa wa Ruvuma, Chadema imepata viti vinne vya Peramiho, Mbinga Magharibi, Mashariki, Madaba na Songea Mjini huku CUF ikichukua majimbi ya Tunduru Kusini, Namtumbo na Tunduru Kaskazini na NCCR Mageuzi wakipata kiti kimoja cha Mbinga Mjini.

Mkoa wa Mwanza Chadema imepata majimbo saba na CUF imepata mawili ya Kwimba na Sumve.

Katika Mkoa wa Kilimanjaro, Jimbo la Vunjo limechukuliwa na NCCR Mageuzi huku yaliyobaki yakichukuliwa na Chadema.

Akizungumza na waandishi wa habari, Naibu Katibu Mkuu NCCR Mageuzi, Nderakindo Kessy, alisema mgawanyo huo umezigatia vigezo walivyojiwekea katika umoja huo na hivyo unapaswa kufuatwa na wagombea wote wa Ukawa.

Alisema mambo ya msingi waliyozingatia katika mgawanyo huo ni matokeo ya ubunge ya mwaka 2010 na kama jimbo lina mbunge ambaye anatokea katika umoja huo jimbo hilo liliachwa katika chama husika hata kama mbunge huyo hataendelea.

“Kigezo kingine ni matokeo ya udiwani ya mwaka 2010, kama chama kina idadi kubwa ya madiwani katika jimbo hilo kinaachiwa na kikiwa na idadi kubwa ya wenyeviti wa serikali za mitaa pia kinaachiwa,”alisema Kessy.

Kessy alisema pia waliangalia mila na desturi ya eneo husika na sifa binafsi pamoja na ubora wa mgombea aliyejitokeza.

“Ieleweke kwamba, mgawanyo huo wa majimbo hautahusiana na mgawanyo wa kata za kugombea udiwani mwongozo wa kuachiana kata ndio utumike katika maamuzi ya kuamua namna ya kugombea katani,” alisema.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Shaweji Mketo alisema watahakikisha Ukawa inashinda si kwa kiti cha urais tu hata majimbo.

Akizungumza katika hafla hiyo ya kubadilishana fomu, Naibu Katibu Mkuu wa NLD, Masudi Makujunga alisema chama chake hakijaenea sehemu kubwa hivyo wanaweza kumudu majimbo matatu.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika alisema waliochukua fomu nje na makubaliano hayo viongozi wa vyama katika umoja huo wahakikishe hazirudishwi.

Akizungumzia suala la kurudisha fomu siku mbili kabla ya tarehe husika, Mnyika alisema tume ya uchaguzi itoe ufafanuzi kauli hiyo na iwe hiari.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles