24.7 C
Dar es Salaam
Thursday, September 12, 2024

Contact us: [email protected]

TPDF yatwaa ubingwa wa ‘hockey’

Na Mwandishi Wetu

TIMU ya mchezo wa mpira wa magongo ( hockey)ya TPDF imetwaa ubingwa wa msimu wa pili wa michuano ya Black Mambaz kwa kuitandika Moshi Khalsa 2-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa jijini Dar es Salaam Jumapili Agosti 11,2024.

Michuano hiyo ilishirikisha timu 13 za mchezo wa mpira wa magongo za Dar es Salaam, Kilimanjaro na Zanzibar huku mechi zikichezwa katika uwanja wa mchezo huo uliopo Lugalo.

Timu ya TPDF, iliyo chini ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ilifika fainali kwa kuifunga Black Mambaz 2-0 katika hatua ya nusu fainali, wakati Moshi Khalsa ilifuzu kucheza fainali ikiifunga Ngome 3-0.

Moshi Khalsa, ambayo pia ni bingwa wa mchezo huo nchini, ilimaliza ikiwa ya kwanza katika kundi B na kukata tiketi ya kucheza nusu fainali huku TPDF ikiongoza kundi A la michuano hiyo na kujihakikishia kucheza nusu fainali.

Mwenyekiti wa Chama cha Mchezo wa Mpira wa Magongo nchini (THA), Kaushik Doshi, amesema katikati michuano hiyo ya siku nne iliandaliwa na klabu ya mchezo huo ya Black Mambaz ya jijini huku ikisimamiwa na THA.

Michuano hiyo, kwa mujibu wa Doshi, ilihusisha timu za wanaume na wanawake, huku timu za wanaume zikiwa nane na timu za wanawake ni tano.

Doshi amesema timu za wanaume ziliwekwa katika makundi mawili, ambapo kundi A liliundwa na Black Mambaz, ambao ni wenyeji, JMK Park, Ngome, na Nyuki ya Zanzibar.

Kundi B lilikuwa na timu za TPDF, KMKM (Zanzibar), mabingwa wa mchezo huo nchini Moshi Khalsa (Kilimanjaro), na Twende Boys.

Doshi ameongeza kuwa michuano iliyozikutanisha timu za wanawake ilishuhudia mechi zikichezwa na wachezaji watano kwa kila timu.

Timu zilizoshiriki katika michuano hiyo ni wakongwe TPDF na Twende Ladies, na timu zenye wachezaji chipukizi za Buza Girls, Black Mambaz Ladies, na Majani ya Chai.

Katika moja ya mechi za siku ya ufunguzi za michuano ya timu za wanaume, wenyeji Black Mambaz walipata ushindi a 4-0 dhidi ya Nyuki katika mechi ya Kundi A.

Mechi yingine ya kundi hili iliyochezwa Ijumaa ilishuhudia JMK Park wakipoteza 2-1 kwa Ngome, moja ya timu zenye uzoefu kutokana na kushiriki michuano mbalimbali wa muda mrefu.

Katika mechi ya Kundi A iliyochezwa siku hiyo hiyo, Ngome walitoka sare ya 2-2 na wenyeji wa michuano, Black Mambaz.

Mechi nyingine ya kundi hilo iliyochezwa Jumamosi asubuhi ilimalizika kwa Nyuki kuichachafya JMK Park na kupata ushindi wa 3-0.

Timu ya JMK Park haikuweza kufua dafu katika mechi nyingine iliyochezwa baadae ambapo ilifungwa 3-1 na Black Mambaz, wakati Nyuki ilitoka sare ya bila kufungana na Ngome.

Mechi za siku ya ufunguzi ya Kundi B iliyozikutanisha timu za Twende Boys na TPDF ilikamilika kwa timu hiyo kongwe ya TPDF kuichapa Twende Boys 11-0.

Wababe wa mchezo wa mpira wa magongo nchini, Moshi Khalsa, walipata ushindi murua wa 3-0 dhidi ya KMKM katika mechi ya kundi hilo iliyochezwa Ijumaa asubuhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles