31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

SHERIA YA ARDHI YAINGIA KWENYE JARIBIO BAGAMOYO

Na Mwandishi Wetu


IMEKUWA kawaida siku zote kwa Serikali kutaka ardhi kutoka kwa wanakikiji  kwa matumizi ya maendeleo, ikiwa tayari kulipia fidia  na wananchi kuhama, lakini kwa mara ya kwanza  kabisa  mamlaka  ya serikali imegomewa na kuleta sintofahamu  kwa wadau wa hatima ya mvutano huo wa nmana yake.

Wanakijiji Bagamoyo wamegoma kuhama kwa namna yoyote  kwenye hifadhi ya Taifa ya Saadani wakidai hawana haja kwani ardhi ni yao na hawako tayari kuhama hata kama Serikali iko tayari kulipa fidia ili kupisha upanuzi wa Mbuga ya Taifa ya  Saadani kwa manufaa makubwa ya uchumi wa watu wa Bagamoyo na Taifa kwa ujumla.

Wananchi wa kitongoji cha Uvinje kilichomo ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Bagamoyo mkoani Pwani, wamegoma kuhama na hawako tayari kuhama wala kulipwa fidia ili kupisha hifadhi hiyo amabayo imeanza kupata umaarafu kwa utalii wa ndani kwa watu wa Dar es Salaam hasa mwishoni  mwa wiki.

Kitongoji  cha Uvinje  kilianza sokomoko hilo na Serikali  kuanzia mwaka 2005, ambapo iliamuliwa kuwa  vijiji vinane hivyo viondolewe kwenye eneo la hifadhi ili kufanya mambo yawe murua baada ya hifadhi hiyo kupandishwa daraja kutoka pori la akiba na kuwa hifadhi kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Namba 281 la Septemba 16, 2005.

Kaimu Mwenyekiti wa Kitongoji hicho, Hassan Akida, alisema mbele ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japheth Hasunga, aliyetembelea hifadhi hiyo kuwa  wakazi wa eneo hilo hawako tayari kuhama na wala kulipwa fidia kwa vile ni ardhi yao toka enzi za mababu zao.

“Tumesema hapa ndiyo  kwetu mnataka kutuhamisha mtupeleke wapi wakati sisi tumezoea maisha yetu hapa,” alihoji  Akida.

Aliongeza kuwa kitongoji hicho kimekuwapo kwa muda mrefu na waliishi bila shida hadi pale pori hilo lilipobadilishwa na kuwa hifadhi ya Taifa.

“Wakati hili ni pori la akiba tuliishi vizuri tu na wazazi wetu walikuwa wafanyakazi wa pori. Lakini tangu iwe hifadhi imekuwa taabu. Sasa tunafukuzwa wakati tumezaliwa hapa na wazazi wetu wamezikwa hapa hapa,” alisisitiza Akida.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Saadani, Adam Mwandosi, alisema mgogoro huo umedumu kwa muda mrefu na umekuwa ukileta chuki kati ya Serikali na wananchi.

Alisema wananchi wa eneo hilo muda mwingine wamekuwa wakimwona hata yeye mwenyekiti wao kama anawasaliti kwa vile tangu mgogoro huo ulipoanza, viongozi wengi wamekuwa wakifika lakini wamekuwa hawana majibu ya kumaliza mgogoro huo.

Hata hivyo, Mhifadhi Mkuu wa Saadani, Stepahano Msumi, amesisitiza kuwa kitongoji hicho kimo ndani ya hifadhi kinyume cha sheria. Alisisitiza kuwa Sheria ya Hifadhi za Taifa hairuhusu makazi ya watu ndani yake.

Wadadisi  wa masuala ya  uhifadhi wanyama  wanadai Mhifadhi amesahau kuwa kwenye Mbuga ya Serengeti Wamasai wanaishi na wanyama  ndani ya Mbuga ya Serengeti na  dhana hiyo kuonekana kivutio kwa watalii, lakini kwa gharama ya mbuga kwani hawaruhusiwi  kulima  chakula na kufanya maendeleo mengine  yoyote ya  maisha  na  hivyo kutegemea Mamlaka ya Hifadhi Wanyama kwa kila kitu.

 

“Kwa ufupi tu ukiangalia Tangazo la Serikali linaonyesha kuwa eneo lote la Kitongoji cha Uvinje liko ndani ya hifadhi. Ni kweli lilikuwa eneo la watu ambao walikuwa watumishi wa Pori la Akiba tangu lilipoanzishwa mwaka 1968. Waliombwa kuondoka lakini waliendelea kuongezeka,” alisema.

 

Historia

Alisema Mhifadhi kuwa katika makubaliano, iliamuliwa kuwa walipwe fidia kwa taratibu lakini hata hivyo licha ya kutekeleza utaratibu wa fidia bado wamegoma kuipokea.

 

Akizungumza mbele ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bagamoyo, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Hasunga, aliwaambia wananchi hao kuwa lengo la ziara yake ni kutaka kuwasikiliza juu ya mgogoro huo na si kuwahamisha.

 

“Mimi ni mgeni kidogo kwenye wizara hii, nimekuja kuangalia si kuwahamisha kwa kuwa sijui eneo hili lina ukubwa kiasi  gani na lina kaya ngapi, lakini nimekuja kutembelea hifadhi na maeneo yote yenye changamoto,” alisema.

 

Alisema amekwenda kuwasikiliza ili aweze kujua jinsi mgogoro ulivyo kwa sababu hakutaka kusikia upande mmoja wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa).

 

Saadani ni hifadhi pekee ya Taifa nchini,  Afrika Mashariki  na Afrika  yenye na mipaka  na fukwe za bahari, kwani  inatazamana na Bahari ya Hindi na fukwe zake zinakutana na uoto wa asili wa nchi kavu wakati  kusini kwake unapita Mto Ruvu  na katikati ya mbuga unapita  mto  Pangani  kwa upande wa Kaskazini.

Hifadhi hiyo inapatikana katika mikoa ya Tanga na Pwani  na uwepo wake ni matokeo ya pori la akiba la Saadani, ranchi ya Mkwaja na sehemu ya kaskazini, sambamba na akiba ya msitu wa asili wa Zaraninge.

 

Kama alivyosema mwenyewe Naibu  Waziri Hasunga, alikuwa anatafiti ukweli wa mambo na ameupata na hivyo atajaribu kutumia Sheria kutekeleza mfumo wa kumaliza tatizo hilo lenye hisia kali kwa wakazi  wake na kufanya maamuzi bila kuogopa upinzani aliouona, kwani Serikali ni moja na si vizuri kuwa na kupindapinda sheria.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles