24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

RC akataa taarifa ya fedha Iyunga

makala1Na Pendo Fundisha, Mbeya

MKUU wa Mkoa wa Mbeya, Amosi Makalla, ameikataa taarifa ya mapato na matumizi ya fedha zilizochangwa na wadau mbalimbali kwa ajili ya ukarabati wa mabweni mawili yaliyoteketea kwa moto katika Shule ya Sekondari ya Wavulana Iyunga.

Kutokana na hali hiyo, Makalla ameuagiza uongozi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya kuiandaa upya taarifa hiyo, kisha kuiwasilisha kwake Aprili 20, atakapokutana na watumishi wa halmashauri hiyo.

Makalla alitoa uamuzi huo katika kikao cha majumuhisho baada ya kusomewa taarifa ya mapato na matumizi na Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Vincent Msolla yaliyotokana na makusanyo ya michango kutoka kwa wadau, baada ya kutembelea na kujionea maendeleo ya ukarabati wa shule hiyo.

Alisema licha ya ukarabati wa shule hiyo kufika hatua nzuri, hajaridhishwa na uandaaji wa taarifa  hiyo kwa kudai imesheheni kasoro nyingi na baadhi ya vitu vilivyotolewa na wadau, havikuthaminishwa kwa thamani ya fedha.

“Kitaaluma mimi ni mhasibu, tena mwenye CPA, nafahamu taarifa za fedha zinavyoandaliwa, mliyoisoma haijakidhi vigezo vya kiuhasibu, nawaombeni mkaiandae upya.

“Hata kanisani watu wakitoa sadaka hutoa fedha na vitu, baadae vitu hivyo huuzwa kwa mnada au kuthaminishwa ili kuona vina thamani gani na kisha kutolewa hesabu ya jumla, hizi figisu  figisu zenu wekeni pembeni nataka taarifa iliyokamilika,” alisema.

Pia alikataa ombi la zaidi ya Sh milioni 100 lililotolewa na Msolla aliyesema fedha hizo zinatokana na deni la vitu ambavyo walichukua kutoka kwa wazabuni mbalimbali wa maduka ya vifaa vya ujenzi.

“Deni hili la Sh milioni 117.5 silitambui, halipo wazi, kwa mujibu wa maelezo yenu mmeeleza tu mnadaiwa kiasi hiki, mmeshindwa kuweka wazi mchanganuo wake,” alisema.

Akitolea ufafanuzi juu ya ujenzi wa mabweni mapya na mengine, Makalla alipinga suala hilo akisema ni matumizi mabaya ya fedha.

Alisema kazi kubwa inayopaswa kufanyika ni ukarabati wa mabweni mawili ambayo yaliteketea kwa moto na yale ambayo miundombinu yake imeonekana kuchakaa.

Februari 29 na Machi 7, mwaka huu, mabweni mawili ya shule ya Iyunga yaliteketea kwa moto na kuharibu mali na vitu vya wanafunzi 151.

Kutokana na hali hiyo, shule hiyo ilifungwa kwa wiki tatu na ilifunguliwa juzi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles