30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NG’OMBE WA MAONYESHO YA NANENANE AIBWA

 

WATU wasiojulikana katika Uwanja wa Maonyesho ya Wakulima na Wafugaji wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, mkoani Morogoro, wameiba ng’ombe wa maonyesho katika banda la Wilaya ya Temeke na kutokomea kusikojulikana.

 

Akizungumza na MTANZANIA Jumamosi jana, Daktari wa Mifugo wa Wilaya ya Temeke, Cleophad Shirima, alisema tukio hilo lilitokea usiku wa saa kumi, Jumatano wiki hii.

 

Alisema mlinzi wa banda hilo ndiye aliyekuwa wa kwanza kubaini kuibiwa kwa ng’ombe huyo, akiwa katika mabanda ya maonyesho.

 

 

Shirima alisema mara baada ya taarifa ya kuibiwa kwa ng’ombe  huyo mkubwa mwenye thamani ya zaidi ya Sh milioni tatu, walitoa taarifa katika kituo kidogo cha polisi ndani ya uwanja huo.

 

“Mara baada ya kutoa taarifa katika kituo hicho walituamuru kwenda kutoa taarifa kituo kikubwa cha polisi kwa ajili ya msako wa ng’ombe huyo,” alisema Shirima.

 

Shirima alisema Jeshi la Polisi limewaambia kuwa linaendelea na uchunguzi ili kubaini wizi huo.

 

Gazeti hili liliwasiliana na Jeshi la Polisi mkoani Morogoro kuhusiana na uhalifu huo na kukiri kupokea taarifa hizo.

 

Aidha, kwa upande wake, Ofisa Habari wa Wilaya ya Temeke, Deyzi Mjinga, alisema matukio ya aina hiyo yanatokana na changamoto za kutokuwapo kwa uzio katika eneo kubwa la uwanja huo wa maonyesho ya wakulima na wafugaji.

 

Alisema mazingira hayo yamekuwa rafiki kwa wahalifu, hivyo kuiomba serikali kulipa kipaumbele cha kwanza suala la ukamilishwaji wa uzio ndani ya uwanja.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles