26.4 C
Dar es Salaam
Wednesday, September 11, 2024

Contact us: [email protected]

MUGABE AMFUKUZA MAKAMU WAKE

HARARE, ZIMBABWE


RAIS Robert Mugabe (93), amemfukuza Makamu wa Rais Emmerson Mnangagwa, hatua inayomsafishia njia mkewe Grace Mugabe kushika wadhifa huo kabla ya kumrithi urais.

Uamuzi huo wa ghafla umekuja siku moja tu baada ya Grace kumtaka mumewe kuchukua hatua hiyo, akimtuhumu bosi huyo wa zamani wa usalama wa taifa kula njama za kutaka kumpindua.

Mwaka 2014, alitoa tuhuma kama hizo zilizosababisha kung’olewa kwa Joice Mujuru ambaye pia alikuwa makamu wa rais.

Mujuru alishiriki vita ya ukombozi dhidi ya wazungu wachache kama ilivyo pia kwa Mnangagwa.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Waziri wa Habari Simon Khaya-Moyo, katika uamuzi wake wa juzi, Mugabe  amemtuhumu Mnangagwa, mshirika wake wa muda mrefu, kwa ukosefu wa utiifu, heshima, ulaghai na kiburi.

Kuondoshwa kwa Mnangagwa kunamaanisha Grace anapewa nafasi kubwa ya kuteuliwa kuwa makamu wa rais katika mkutano maalumu wa chama tawala cha Zanu-PF utakaofanyika mwezi ujao.

“Mke wa Rais ana nafasi nzuri ya kujaza wadhifa wa Makamu wa Rais na ana uungwaji mkono mkubwa ndani ya vikao muhimu vya Zanu-PF,” alisema  Tinashe Jakwa, mchambuzi wa Taasisi ya Masomo ya Kiafrika ya Australia na Pacific (AFSAAP).

Hata hivyo, katiba kwa sasa hairuhusu mwanamke kuwa makamu wa rais, hivyo itapaswa kwanza kurekebishwa na tayari mabaraza ya majimbo yameeleza utayari wa kufanya hivyo.

Agosti mwaka huu, Grace alituhumiwa kumshambulia mwanamitindo Gabriella Engels nchini Afrika Kusini, lakini akaruhusiwa kurudi Zimbabwe baada ya Serikali ya Afrika Kusini kuridhia kinga ya kibalozi kutoka Serikali ya Zimbabwe, hatua ambayo ililalamikiwa na wanaharakati na wanasiasa nchini humo, waliotaka achukuliwe hatua.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles