24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Msigwa kuanika madudu mengine Maliasili

Mchungaji Peter Msigwa
Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa

NA AZIZA MASOUD, DAR ES SALAAM

MBUNGE wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa, ameahidi kuweka hadharani madudu mengine yanayofanywa na kampuni mbalimbali zilizopewa leseni za uwindaji nchini kwa usimamizi wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mchungaji Msigwa, ambaye pia  ni Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, ametoa kauli hiyo baada ya juzi Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, kufuta umiliki wa vitalu vilivyo chini ya kampuni ya uwindaji ya Green Miles Safaris Ltd.

Uamuzi huo wa Nyalandu ulitokana na hatua ya Msingwa kuonyesha video ya jinsi Kampuni ya Uwindaji ya Green Miles Safari Ltd. inavyokiuka sheria za uwindaji kwa kutesa wanyamapori.

Hatua ya Wizara kuifutia umiliki wa vitalu kampuni hiyo inatoa onyo kwa kampuni nyingine za kitalii za uwindaji zinazokiuka sheria za nchi.

Kutokana na hilo, Msigwa alimpongeza Waziri Nyalandu kwa kuwa waziri wa kwanza kufuata ushauri wa wapinzani.

“Nampongeza Waziri Nyalandu kwa hatua aliyochukua na kuwa waziri wa kwanza kuchukua ushauri wa kutoka upinzani kwenye masuala muhimu ya kulinda maliasili zetu,” aliandika Msigwa katika ukurasa wake wa Facebook.

Pamoja na hilo, Msigwa amemuomba  Waziri Nyalandu  kutoishia kwenye hatua hiyo tu, ila afanye uchunguzi wa kina kwa makampuni yote ya uwindaji ili kuhakikisha sheria, taratibu na kanuni za uwindaji zinafuatwa.

Kwa mujibu wa Nyalandu, vitalu vya uwindaji vilivyofutiwa leseni sambamba na vibali vyote vya uwindaji vilivyotolewa katika msimu huu ni pamoja na Lake Natron GC East, Gonabis/Kidunda-WMA na MKI-Selous.

Wakati akitangaza uamuzi huo dhidi ya kampuni hizo, Nyalandu aliyataja makosa yaliyofanywa na Kampuni ya Green Mils Safari ni kuwinda wanyama ambao hawakuruhusiwa kwenye leseni, wakiwamo nyani na ngedere kifungu na kwamba ni kinyume na kifungu cha sheria cha 19(1)(2) ya kuhifadhi wanyamapori ya mwaka 2009.

Hatua hiyo ambayo Mchungaji Msigwa aliita kuwa ni kubwa kimaamuzi, alisema kwa sasa anaamua kukaa kimya, huku akiendelea na uchunguzi ambao utaibua mambo mengine mapya hivi karibuni.

“Kwa sasa nanyamaza kwa sababu haya mambo ya ujangili ni mazito, hatua aliyoifikia waziri husika si kitu kidogo, ila nitaongea tena wiki ijayo,” alisema Mchungaji Msigwa.

Katika hilo, alisema uchunguzi anaoufanya katika baadhi ya mambo utakuwa kama ushahidi katika masuala mbalimbali atakayoyaongea siku hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles