29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Mgimwa apata mpinzani mpya jimbo la Kalenga 

M2Na Elias Msuya

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo kimepata mgombea mpya atakayepambana na mgombea wa CCM katika jimbo la Kalenga katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Jimbo hilo linaloshikiliwa na Godfrey Mgimwa aliyeshinda uchaguzi mdogo Machi 2014 baada ya baba yake mzazi, Dk. William Mgimwa, kufariki dunia.

Akizungumza jana katika mkutano wa hadhara katika kijiji cha Kidamali, Kalenga Iringa vijijini, mgombea mpya wa Chadema anayewakilisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Dk. Mussa Mdede alisema yukop tayari kulitoa jimbo hilo mikononi mwa CCM.

Mdede ambaye ni daktari kitaaluma alisema kwa kipindi ambacho Mgimwa amekuwa mbunge wa jimbo hilo hakuna alilofanya zaidi ya kuonyesha dharau kwa wananchi.
“Sijagombea ubunge ili nikavae tai na kula bata Dodoma. Tangu nimeanza kampeni huyu mwenzangu amesema hana sababu ya kuanza kampeni. Eti ataweka koti tu. Hivi koti na mtu nani muhimu? Lazima tuonyeshe nani ni nani,” alisema Mussa.

Alisema CCM haina mpango wowote na Jimbo la Kalenga kwa sababu imeshindwa kutatua kero ya uhaba wa maji, kilimo na afya.

“Kwa mujibu wa sera ya afya tuna vijiji 75, tunatakiwa kuwa na zahanati 75, hivyo tuna upungufu wa zahanati 34, upunguvu vituo vya afya 12, vipo vitatu.

“Hatuna hospitali ya wilaya, ile iliyopo ni ya Wakatoliki, hata mipra ya kusaidia wagonjwa haipo. Ipamba ndiyo Muhimbili inahudumia Iringa vijijini yote,” alisema Mdede.

Alisema japo viongozi wa CCM wanawaita wananchi wapumbavu malofa bado Serikali inaedelea kuwadai michango ya maabara ili hali inafuja fedha kwa kashfa za ufisadi.
“Leo wanatudai michango ya maabara. Hela ya Escrow waliyoiba ingeweza kumaliza madawati na kujenga maabara. Tuliambiwa maisha bora kwa kila Mtanzania tangu Rais Kikwete alipochukua madaraka mwaka 2005 lakini gharama za maisha zimepanda. Watu wa Kalenga tuseme inatosha.

Alitaja kero nyingine kuwa ni uhitaji wa wananchi wa kijiji hicho kukifanya kuwa halmashauri ya mji mdogo, lakini imeshindikana kwa sababu ya rushwa, akisema atatatua kero hiyo.

“Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari alichukua shamba lililokuwa halitumiki akawapa wananchi wake maeneo ya kutumia. Tutachukua ardhi ambazo hazitumiki na kuwapa wananchi watumie. Tuchagueni Ukawa kwasababu oil chafu huondoa mchwa,” alisema Mdede.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Zanzibar), Said Issa alisema Kalenga ni jimbo linalozalisha aina karibu zote za mazao lakini kilimo kimeshindikana.
Alisema kutokana na hali hiyo Ukawa watatoa ruzuku kwa wakulima ili wanufaike.

“Katika utawala wetu tutatoa elimu bure kwa ngazi zote. Si kama CCM wanaosema watatoa elimu bure wakati mnaendelea kulipishwa. Dk. John Magufuli anaendelea kuahidi wakati alikuwa ndani ya Serikali kwa miaka 20,” alisema Issa.

Naye mgombea mwenza wa urais wa Ukawa, Juma Duni Haji aliwataka wapiga kura wa Kalenga kutokuwa waoga wa kuleta mabadiliko siku ya kupiga kura.

“Tabia ya hofu mwondoe. Watu wanatishwa, CCM wanapita na kuwaendea wale wenye shida watu wazima, wanawadhalilisha sana na kuwagawia vijisenti, wanachukua vitambulisho vyao na kuwagawia madira. Hakuna sababu ya kumwogopa mtu wa Kalenga na wewe umezaliwa Kalenga,” alisema Duni.

Alisema mabadiliko yanayoletwa na Ukawa si ya kubadilisha wagombea bali ni kubadilisha mfumo wote wa CCM na kuongeza kuwa njia pekee ya kuleta mabadiliko ni kutoa elimu bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles