23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

MCHELE WAPANDA BEI DAR

Na CHRISTINA GAULUHANGA

DAR ES SALAAM

WAKATI baadhi ya bidhaa za nafaka zikianza kushuka bei katika masoko mbalimbali, mchele unapanda bei kwa kasi.

Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA katika masoko mbalimbali jijini Dar es Salaam umebaini katika kipindi cha miezi mitatu bei ya mchele imeanza kuongezeka hali inayotishia walaji na wafanyabiashara.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa Wauza Nafaka na Wawekezaji wa Soko la Tandale (Tamagrasai), Juma Dikwe, alisema bei ya mchele imeanza kupanda kwa sababu baadhi ya mikoa inayozalisha mpunga kwa wingi haikupata mavuno ya kutosha msimu huu.

“Kadri siku zinavyokwenda mchele utazidi kupanda bei kabisa kwa sababu wenzetu wa Shinyanga mwaka huu hawajaambulia kitu kwa upande wa mpunga,”alisema Dikwe.

Alisema bei ya chini ya mchele ilikuwa Sh1,300 imeongezeka na kufikia Sh1,600 hadi Sh 2,000 na kadri siku zinavyoongezeka utazidi kupanda zaidi.

“Kwa sasa tunategemea mchele kutoka mkoani Morogoro na Mbeya hivyo ni imani yetu gharama ya mchele itazidi kupanda kwa sababu ya ukubwa wa mahitaji ya watumiaji,”anasema Dikwe.

Kwa upande wa mahindi, mwenyekiti huyo alisema inazidi kushuka kwa kasi tofauti na siku zilizopita.

Aliitaja bei ya awali kuwa ilikuwa Sh 1,000 kwa kilo moja ya mahindi lakini kwa sasa imefika Sh 500 katika masoko mbalimbali.

Dikwe alisema kwa upande wa bidhaa za ngano kilo moja inauzwa Sh  1,200, karanga  Sh 2,200 na ulezi umepanda hadi kufikia Sh 2,200.

Hata hivyo aliiomba Serikali kuendelea kudhibiti uuzaji wa mahindi nje ya nchi kwa sababu itasaidia Watanzania kupata mahindi kwa wingi na kwa bei nafuu.

MTANZANIA ilitembelea soko la Tandale, Buguruni na Kariakoo na kuzungumza na baadhi ya wafanyabiashara kwa nyakati tofauti ambao walilalamikia upatikanaji wa mchele umekuwa adimu.

Mfanyabiashara, Abuu Seleman wa Soko la Kariakoo alisema, kadri wanavyokwenda kuchukua mzigo mpya wa mchele wanakuta bei imeongezeka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles