25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Mafuriko yaharibu kiwanda, makazi Moshi

NA RODRICK MUSHI, MOSHI
ZAIDI ya kaya 700 katika Kata ya Arusha Chini TPC, Wilaya ya Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro, hazina makazi baada ya nyumba zao kuharibiwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyonyesha juzi.
Pamoja na madhara hayo kwa wananchi, pia mafuriko hayo yameharibu miundombinu ya Kiwanda cha Sukari cha TPC, taasisi mbalimbali pamoja na mashamba ya mazao ya chakula.

Taarifa hiyo ilitolewa jana na Ofisa Mtendaji na Utawala wa Kiwanda cha TPC, Jaffari Ally, alipokuwa akitoa taarifa kwa Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Novatus Makunga, aliyetembelea maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko hayo.
“Kwa eneo langu la kiwanda, wafanyakazi wangu zaidi ya 600 hawana makazi na ukija kwenye miundmbonu ya kiwanda, imeharibiwa kwa kiwango
kikubwa kwani barabara, reli pamoja na mashamba yameharibiwa pia.
“Kwa ujumla, mafuriko haya yamechangiwa na mvua kubwa iliyonyesha mkoani Arusha na hapa Kilimanjaro kwa ukanda wa juu kwani eneo hilo lina makutano ya Mito ya Weruweru, Karanga na Kikavu,” alisema.
Naye, Makunga alisema wananchi walioathiriwa na mafuriko hayo wako katika Vijiji vya Kata ya Arusha Chini TPC ambavyo ni River Side, Kijiji cha
Kati, Langasani Magharibi na Mashariki.

“Kwa asilimia kubwa, maji yaliyosababisha mafuriko haya yametokana na mvua iliyonyesha Mkoa wa Arusha na mito mingi ilishindwa kuyahimili na hivyo kingo kuharibika na maji kuvamia makazi ya watu.

“Hata hiyo, hasara iliyotokana na mafuriko haya kwa upande wa kiwanda cha sukari pamoja na wananchi, bado haijajulikana kwa sababu tathmini bado inaendelea,” alisema Makunga.
Kutokana na uharibifu uliotokea, alisema wananchi walioharibiwa makazi yao wamehifadhiwa katika sehemu ya kiwanda cha TPC ambayo haikuathiriwa.
Kwa upande wake, mdau wa maendeleo katika Jimbo la Moshi Vijijini, Ansi Mmasi, alisema kuna haja ya Serikali kuangalia namna ya kukabiliana na mafuriko hayo kabla hayajaleta madhara zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles