24.1 C
Dar es Salaam
Sunday, September 8, 2024

Contact us: [email protected]

MADEREVA BODABODA HATARINI KUPOOZA

img_1409

Na VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

MADEREVA wa pikipiki, maarufu bodaboda, wapo katika hatari ya kuharibikiwa mfumo wa fahamu, kupooza na kupata kifafa miaka ijayo, imeelezwa.

Hali hiyo inachochewa zaidi na ongezeko la matukio ya ajali ambazo wamekuwa wakizipata kila siku wakiwa barabarani.

Daktari bingwa wa magonjwa ya ubongo na mishipa katika Kitengo cha Mishipa ya Fahamu (Neurology) wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Patience Njenje, alisema hayo jana, alipozungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu.

“Ni hatari ambayo tunaona kama hatua hazitachukuliwa ndugu zetu hawa watakuwa na wakati mgumu, wengi wanaumia kichwani, tatizo wanaendesha bila kuzingatia sheria na hawavai kofia ngumu kujikinga.

“Unajua jinsi Mwenyezi Mungu alivyoumba ubongo, umefunikwa na fuvu ambalo limeundwa na vitu mfano wa karatasi (layers) nyingi ambazo kazi yake ni kuukinga ubongo kwa kuzuia kitu chochote kigeni kuingia ndani.

“Sasa mtu anapata ajali na akawa amejipiga kichwani, ubongo wake huweza kupata tatizo, wapo ambao baadaye miili yao hupata stroke ‘kupooza’ au kuwa na kifafa,” alisema.

Dk. Njenje alisema matatizo ya ubongo kitaalamu hugawanywa katika makundi mawili, ‘organic’ yaani nyama ya ubongo na ‘in-organic’ yaani utendaji wa ubongo.

“Tunapozungumzia ‘organic’, tunaeleza moja kwa moja mambo yanayochangia kuharibu mfumo wa ubongo, ikiwamo ajali, matumizi ya kemikali, magonjwa yasiyokuwa ya kuambukiza, magonjwa ya kurithi na wadudu (infections).

“Iwapo mdudu wa ugonjwa kwa mfano malaria akapenya na kuingia kwenye ubongo, ndipo pale utasikia madaktari wakisema malaria imepanda kichwani,” alisema.

Alisema wanawake wanaotumia dawa za nywele nao hujiweka katika hatari kwani nyingi huenda kuharibu mfumo wa ubongo.

“Baadhi ya dawa zina kemikali kali, kwa mfano zebaki na steroids, hizi huharibu afya ya ubongo, kwa kweli hali ni mbaya kwani wagonjwa ni wengi, kila siku Muhimbili tunaona wagonjwa 40 wanaofika kufanya kipimo cha EEG, ambacho hutumika kupima umeme wa ubongo. Wagonjwa ni wengi, tumeelemewa,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles