23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

LOWASSA, MBOWE SUMAYE WAANZA ZIARA MIKOANI

pg-4

VIONGOZI waandamizi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wanaendelea na ziara ya kazi inayohusisha vikao vya ndani katika majimbo ya Kanda ya Kati.

Kanda hiyo inajumuisha mikoa ya Morogoro, Dodoma na Singida na   inaongozwa na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa chama hicho, Tumaini Makene, alisema hayo jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari.

Alisema ziara hiyo ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi wa ndani ya chama hicho kwa kanda hiyo ambao unatarajiwa kufanyika Novemba 23, mwaka huu.

img-20161120-wa0052

“Mwenyekiti Mbowe anaongoza timu inayokwenda katika majimbo ya Mkoa wa Morogoro, akiambatana na Mjumbe wa Kamati Kuu Profesa Mwesiga Baregu, ambako jana (juzi) walikuwa katika majimbo ya Mlimba na Kilombero na leo (jana) wamefika majimbo ya Mikumi na Kilosa,” alisema.

Makene alisema Makamu Mwenyekiti wa Chama  (Tanganyika), Profesa Abdalla Safari anaongoza timu iliyopo mkoani Dodoma, akiambatana na Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri Mkuu Mstaafu Edward Lowassa   na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalim.

“Jana (juzi) walifika majimbo ya Kongwa na Mpwapwa na leo (jana) walifanya ziara katika majimbo ya Chemba na Kondoa,” alisema.

Alisema timu ya tatu inaongozwa na Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika akiambatana na Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye.

“Timu hii jana (juzi)  walikuwa katika majimbo ya Singida Mashariki, Singida Magharibi, Singida Mjini na Singida Kaskazini na leo (jana) walifika majimbo ya Manyoni Mashariki na Manyoni Magharibi (Singida) na Bahi (Dodoma),” alisema.

Makene alisema katika ziara hiyo, viongozi wakuu pamoja na wajumbe wa kamati kuu wameambatana na wabunge ambao wamegawanywa katika timu mbalimbali na kupangiwa majukumu kwenye kanda nane za upande wa Tanganyika, kati ya Kanda 10 za chama nchi nzima.

“Novemba 22, mwaka huu  (leo) timu zote zitaendelea na ziara katika majimbo mengine katika mikoa hiyo mitatu kadri ya ratiba ya ziara nzima ilivyopangwa.

“Novemba 23, mwaka huu wajumbe wa Baraza la Uongozi la Kanda ya Kati watakutana kwa ajili ya kikao cha uchaguzi, kuchagua mwenyekiti, makamu mwenyekiti na mweka hazina wa kanda,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles