33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Kigogo Rita atumia mgongo wa Chenge kukwepa Escrow

FREDY AZZAH NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
OFISA Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufilisi na Udhamini (Rita), Philip Saliboko, anayetuhumiwa kupata mgawo wa Sh milioni 40 za Akaunti ya Tegeta Escrow, ametumia mbinu zilizotumiwa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge (CCM), kukwepa kuhojiwa na Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma.
Hatua hiyo imekuja siku chache baada ya Chenge kukataa kuhojiwa na Baraza hilo Februari 25, mwaka huu, akisema kuna zuio la Mahakama Kuu linalokataza suala hilo kujadiliwa na chombo chochote.
Baada ya pingamizi hilo, Februari 26, mwaka huu, Baraza hilo lilitoa hukumu ndogo juu ya pingamizi hilo na kusema zuio la Mahakama Kuu halilizuii kujadili suala hilo.
Sababu ya pili ya Baraza kutupilia mbali pingamizi hilo, ni kutokana na kile lilichosema zuio la Mahakama Kuu kuzuia mjadala huo ambao matokeo yake yatafanya jambo hilo lijadiliwe kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano, jambo ambalo halitatokea kwa baraza hilo kumhoji mtuhumiwa.
Hata baada ya maelezo na msimamo huo wa Baraza, Chenge alikataa kuhojiwa na kutaka kwenda Mahakama Kuu kutafuta tafsiri ya zuio hilo.
Njia hiyo ya Chenge kukwepa mkono wa Baraza hilo, ndiyo iliyotumiwa na Saliboko jana ambaye baada ya kusomewa mashtaka yake aliyakana.
Baada ya kuyakana, wakili wake, Jamhuri Johnson, aliomba kutojadiliwa na Baraza hilo kwa madai kuna zuio la Mahakama Kuu linalokataza shauri linalohusu Kampuni ya Kufua Umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) na miamala ya Akaunti ya Tegeta Escrow kujadiliwa.
“Pamoja na kuwa kwenye shauri la Chenge, Baraza hili lilisema lina uwezo wa kusikiliza shauri hili na kwamba lenyewe siyo sehemu ya zuio lililo Mahakama Kuu, tunasema kwamba zuio lililo Mahakama Kuu linahusu vyombo vya umma, na hili Baraza ni chombo cha umma.
“Kwahiyo tukatafsiri kwamba, ‘by necessary implication’, kama vyombo vingine vya umma vimezuiwa kujadili hili suala, basi na hili Baraza limezuiwa kwa sababu ni chombo cha umma,” alisema.
Baada ya kusema hayo, wakili wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Hassan Mayunga, alipinga pingamizi hilo kwa madai kuwa Baraza hilo lilishatolea ufafanuzi suala hilo.
Alisema Baraza hilo ni chombo kinachojitegemea na kwamba hakiwezi kuzuiwa kulijadili suala hilo.
“Amri hiyo si zuio la dunia nzima na wala halizuii watu wengine, bali mwanasheria anatengeneza kichaka kukwepa majukumu yake ya kisheria,” alisema Mayunga.
Baada ya mabishano ya mawakili hao, Mwenyekiti wa Baraza hilo, Jaji mstaafu Hamis Msumi, aliitupilia mbali hoja ya wakili wa Saliboko.
Katika kuitupa hoja hiyo, Jaji Msumi alisoma tena hukumu ndogo aliyoitoa alipokuwa akiamua pingamizi la Chenge.
Jaji Msumi alisema zuio la Mahakama Kuu, mkazo uliwekwa katika kulijadili suala hilo na kusababisha liwasilishwe bungeni.
Alisema kutokana na hali hiyo, pingamizi hilo halina msingi, kwani pia Baraza hilo linajitegemea na huru na siyo kati ya vyombo vilivyozuiwa na mahakama hiyo kujadili suala hilo.

MASHTAKA YA SALIBOKO
Akisoma mashtaka yanayomkabili Sariboko, Wakili wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Mayunga, alisema mlalamikiwa amekiuka maadili ya viongozi wa umma kwa mujibu wa fungu la 12 (1) e, 12 (2) na fungu la 6 (f) ya sheria ya maadili ya mwaka 1995.
“Mlalamikiwa aliomba fadhila za kiuchumi kutoka kwa James Rugamalira kinyume cha fungu la (6) (f) ya sheria ya maadili ya viongozi wa umma ya mwaka 1995, ambalo linamzuia kiongozi wa umma kuomba au kupokea fadhila za kiuchumi,” alisema.
Alisema mlalamikiwa alipokea Sh 40,429,000 kutoka Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited.
“Fedha hizo ziliingizwa katika akaunti ya mlalamikiwa iliyoko Benki ya Mkombozi, tawi la St. Joseph, Dar es Salaam, akaunti namba 00420102645501, Februari 5 mwaka 2014,” alisema.
Alisema mlalamikiwa kwa wadhifa wake wa Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Ufilisi (Rita), aliteuliwa na Mahakama Kuu kuwa mfilisi wa muda wa mali za IPTL, kampuni ambayo VIP Engineering and Marketing Limited ilikuwa inamiliki hisa asilimia 30.
“Kitendo cha mlalamikiwa kupokea Sh 40,429,000 kutoka kwa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited, iliyokuwa na hisa kwenye Kampuni ya IPTL, wakati mlalamikiwa akiwa mfilisi wa mali za IPTL, ni ukiukwaji wa fungu la 6 (e) la sheria ya maadili ya viongozi wa umma, ambalo linamzuia kiongozi wa umma kujiingiza katika mgogoro wa masilahi,” alisema.
Alisema mlalamikiwa kwa kutumia wadhifa wake, alijipatia manufaa ya kifedha kinyume na fungu la 12 (1) (e) la sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
“Mlalamikiwa hakutamka jumla ya Sh 40,429,000 alizopokea kutoka kwa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited kinyume na matakwa ya fungu la 6 (e) na fungu la 12 (2) la sheria ya maadili ya viongozi wa umma,” alisema wakili Mayunga.

MUJUNANGOMA KUSUBIRI KESI YA KISUTU
Katika hatua nyingine, Baraza hilo limekubali pingamizi la kutosikiliza kesi ya Mkurugenzi wa Huduma za Sheria katika Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rogonzibwa Mujunangoma, hadi pale kesi ya jinaidi kuhusu uchotwaji wa fedha hizo iliyo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu itakapokwisha.
Mujunangoma alifikishwa mbele ya Baraza hilo akidaiwa kujipatia manufaa ya kifedha kiasi cha Sh 423,400,000 kwa ushauri anaoutoa katika Kampuni ya VIP na Mabibo Beer Wines and Sprit kinyume cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
Pingamizi lake la kutojadiliwa na Baraza hilo kutokana na kuwa na kesi inayohusu suala hilo mahakamani, lilikubaliwa jana baada ya Jaji Msumi kusema hoja zilizotolewa na mlalamikiwa ni za msingi.
Jaji Msumi alisema hoja ambayo imeonekana kuwa na msingi wa kisheria iliyochangia kulishawishi Baraza kukubali pingamizi hilo, ni ukweli kwamba mashtaka yaliyoko Kisutu ndiyo yale waliyomfungulia katika Baraza la Maadili.
“Sheria inakataa mshtakiwa kuwa na kesi katika sehemu mbili kwa wakati mmoja yenye malengo yaleyale kwenye vyombo tofauti, inamkosesha nafasi ya kujitetea,” alisema.

MASHTAKA
Kabla ya pingamizi lake kukubaliwa, Mujunangoma alikuwa akikabiliwa na mashtaka ya kutoa ushauri wa kisheria katika Kampuni ya VIP na Mabibo Beer Wines and Sprit kinyume cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma na kujipatia manufaa ya kifedha kiasi cha Sh 423,400,000.
Pia kuingiziwa fedha katika akaunti yake yenye namba 00120102602001 iliyopo kwenye Benki ya Mkombozi, Tawi la St. Joseph, Dar es Salaam.
Kwa kitendo cha mlalamikiwa kuwa mshauri wa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited ambayo ilikuwa na hisa za asilimia 30 katika Kampuni ya IPTL ni kujiingiza katika migongano ya kimaslahi.
Kosa jingine ni mshtakiwa kutotamka masilahi aliyokuwa nayo katika mkataba wa Tanesco na IPTL kupitia Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited kinyume cha matakwa ya kifungu cha 14 cha sheria ya maadili.
Mlalamikiwa kutotamka madeni yake aliyokuwa anaidai Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Limited na Mabibo Beer Wines and Sprit kwa kamishna wa maadili kwa kipindi cha mwaka 2013 kinyume na matakwa ya kifungu cha 9(6)(b) cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles