27 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Kagame avunja Baraza la Mawaziri

Paul Kagame
Rais wa Rwanda, Paul Kagame

RAIS wa Rwanda, Paul Kagame, amevunja baraza lake la mawaziri kwa kumuondoa aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Dk. Pierre Damien Habumuremyi na kumteua aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma wa nchi hiyo, Anastase Murekezi, kuchukua wadhifa huo.

Dk. Habumuremyi alikuwa Waziri Mkuu wa Ruwanda tangu Oktoba 7, mwaka 2011.

Murekezi amekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo tangu kumalizika vita vya mauaji ya kimbari mwaka 1994.

Waziri Mkuu wa kwanza alikuwa Faustin Twagiramungu, akifuatiwa na Pierre Celestin Rwigema na badaye Bernard Makuza.

Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Rwanda, Ibara ya 117, Waziri Mkuu mpya mteule anatakiwa kuunda Baraza jipya la Mawaziri ndani ya kipindi kisichozidi siku 15 tangu uteuzi wake.

Katika kifungu cha 124 cha katiba hiyo, kinaruhusu Serikali kuendelea na shughuli zake za kila siku hadi baraza jipya la mawaziri liundwe.

Mara baada ya uteuzi huo, waziri mkuu mpya kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Twitter alisema: “Ni heshima kubwa kwangu kuteuliwa kuwa waziri mkuu wa Jamhuri ya Rwanda.

Ninamshukuru rais kuniteua kuwa waziri mkuu. Wadhifa huu mpya ni nafasi ya pekee kuendelea kulitumikia taifa na Wanyarwanda wote tufanye kazi kwa bidii pamoja.”

Naye Dk. Habumuremyi alisema: “Shukrani zangu za dhati kwa Rais Paul Kagame na RPF kwa kuniamini na kuniteua kuwa waziri mkuu na wote mlioniunga mkono. Mungu awabariki.”

Dk. Habumuremyi alizaliwa wilayani Musanze, kaskazini mwa Rwanda mwaka 1961 na kusoma vyuo vikuu vya Kongo Kinshasa, Ufaransa na hatimaye Shahada ya Uzamivu (PhD) ya Sayansi ya Siasa kwenye Chuo Kikuu cha Ouagadougou, Burkina Faso mwaka 2011.

Miongoni mwa kazi alizofanya ni kufundisha Chuo Kikuu cha Rwanda, nyadhifa za juu kwenye taasisi binafsi na kabla ya kuwa waziri mkuu alikuwa Waziri wa Elimu wa Rwanda.

Murekezi alizaliwa mwaka 1952 na kabla ya uteuzi wake alikuwa waziri wa utumishi wa umma. Kitaaluma ni Mhandisi wa Kilimo, amesoma Chuo Kikuu cha Louvain-La Neuve, Ubelgiji.

- Advertisement -

Related Articles

1 COMMENT

  1. Viongozi wa CCM wasijifanye hawajui chanzo cha tatizo lililoko katika bunge la katiba.Kuna mtu hadi leo hii hajui kuwa Rais ni chanzo cha tatizo?Kuna mtanzania asiyejua kuwa CCM ni tatizo?Cha kushangaza UKAWA ndio wanaohamishiwa tatizo.Kwa nini ninyi viongozi msijiondoe kwenye unafiki kwa kusema ukweli juu ya mwenyekiti wenu kwa kuvuruga mchakato mzima wa katiba?Ni huto tu vyeo alitowapa?Acheni unafiki!

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles