27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

JPM: CCM MSIWAOGOPE WATENDAJI WA SERIKALI

Na MAREEGSI PAUL-DODOMA


MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dk. John Magufuli, amewataka viongozi wa chama hicho, wasiwaogope watendaji wa Serikali kwa kuwa Serikali wanayoiongoza iko chini ya chama chao.

Magufuli alitoa maagizo hayo mjini hapa jana, alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa tisa wa chama hicho.

“Hayati Mwalimu Nyerere, aliwahi kusema kwamba kazi ya chama ni kuwaunganisha wananchi na Serikali yao.

“Kwahiyo, lazima watendaji wa Serikali wajue mipango ya Serikali yao na nitashangaa kama wananchi watalalamika juu ya umuhimu wa ununuzi wa ndege, ujenzi wa reli na mambo mengine wakati kiongozi wa CCM yupo, nitashangaa sana.

“Kwahiyo, nawataka viongozi wa Chama Cha Mapinduzi, msiwaogope watendaji wa Serikali, hasa hasa katika kutetea masilahi ya wanyonge, kwa sababu CCM ndicho chama tawala na viongozi wote wako chini yake,” alisema.

Akizungumzia ukosoaji wa mambo ndani ya Serikali, alisema wana CCM wanaruhusiwa kukosoa, lakini wanatakiwa kujua uchungu wa mwana, aujuaye mzazi.

Kwa mujibu wa Magufuli, wana CCM wanapotaka kuikosoa Serikali, wanatakiwa kukumbuka wao ni wana CCM na wajue namna ya kukosoa.

“Ndani ya CCM tuna utaratibu wa kukosoana, lakini mnapokuwa mnaikosoa Serikali, kumbukeni kuna njia nyingi za kukosoa na mjue uchungu wa mwana aujuaye mzazi,” alisema.

Akiwazungumzia Makamu Mwenyekiti wa CCM (Zanzibar), Dk. Ali Mohamed Shein na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara), Philip Mangula, alisema wamekuwa wakimsaidia katika utendaji wake wa kazi kutokana na uzoefu wao katika siasa.

“Kwa dhati ya moyo wangu, nawapongeza sana Dk. Shein na Mangula kwa sababu wamekuwa wakinisaidia sana tena sana, japokuwa wakati mwingine watu wanasema Mangula ni kama Mugabe.

“Huwezi kuongoza chama bila wazee kama hawa, wazee ni muhimu, ndiyo maana bado tunao akina mzee Mwinyi, mzee Mkapa na mzee Kikwete.

“Mimi bado ni kijana kidogo kidogo na kuna wakati nachemkaga kidogo, lakini hawa wazee wananisaidia sana. Mzee mwingine anaitwa Kinana (Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana), mnaweza kumuona kama ni kijana kwa sababu amenyoa nywele.

“Huyu amenisaidia sana kufanya reform (mageuzi) ndani ya chama na mategemeo yangu ni kwamba ataendelea kunisaidia,” alisema Magufuli huku akishangiliwa baada ya kumtaja Kinana.

Pamoja na hayo, Magufuli aliendelea kusisitiza kwamba maendeleo hayana chama ingawa anaamini maendeleo ya kweli yanapatikana kupitia CCM.

Wakati huo huo, Dk. Magufuli alizidi kukemea rushwa ndani ya chama na kusema viongozi watakaokiuka maadili, watachukuliwa hatua bila kujali vyeo vyao.

Kuhusu viongozi walioshinda katika chaguzi mbalimbali ndani ya chama hicho, aliwataka wafanye kazi kwa uadilifu, wawatembelee wanachama wote na wahakikishe wanaongeza wanachama wapya ili chama kizidi kuwa na idadi kubwa ya wanachama.

Aliwataka pia walioshindwa wasiendelee na makundi waliyokuwa nayo wakati wa uchaguzi, kwa kuwa katika uchaguzi kuna kushindwa na kushinda.

Pia, Dk. Magufuli alieleza kwa kifupi hali ya usalama wa nchi na kusema iko salama na waliokuwa wakitaka kuvuruga muungano, walichukuliwa hatua kadiri ilivyowezekana.

 

HAMAHAMA NA KIMBUNGA

Akizungumzia wanasiasa wanaohama vyama vyao na kujiunga na CCM, Dk. Magufuli alisema amepata taarifa kuna mbunge mmoja anataka kujiunga na chama hicho akiwa na madiwani saba.

“Kuna viongozi wengine wanataka kurudi CCM na wasaidizi wangu wameniambia kuna mbunge mmoja anataka kurudi na madiwani saba wa kwenye jimbo lake.

“Hiki ni kimbunga na nawaambia wataisoma namba. Mimi ni yule yule, nawapenda sana na bado nakipenda Chama Cha Mapinduzi,” alisema Dk. Magufuli huku wajumbe wa mkutano huo wakishangilia.

Alisema wapo wabunge wengi ambao wanataka kujiunga na CCM, lakini wanaendelea kuwachuja ili kujiridhisha.

Kutaka kuhama kwa mbunge huyo ni mwendelezo wa wabunge wa upinzani kuhamia CCM.

Tayari wabunge wawili wa upinzani wameshahamia CCM wakitoka CUF na Chadema.

Wanachama hao wapya wa CCM ni aliyekuwa Mbunge wa Kinondoni mkoani Dar es Salaam, Maulid Mtulia kwa tiketi ya CUF na wa Siha mkoani Kilimanjaro, Dk. Godwin Mollel (Chadema).

Hivi karibuni mbunge wa zamani wa Kigoma Kusini, David Kafulila pia alijiunga na CCM akitokea Chadema.

Wengine waliojiunga na chama hicho kutoka Chadema na ACT- Wazalendo ni Albert Msando, Samson Mwigamba, Edna Sunga, Lawrence Masha, Patrobas Katambi, Profesa Kitila Mkumbo na Anna Mghwira.

 

KINANA

Naye Kinana alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za chama kuanzia mwaka 2012 hadi 2017, alianza kwa kusema hawezi kumkatalia mwenyekiti wake kwa kuwa ameonyesha nia ya kutaka kuendelea kuwa naye madarakani………

Kwa habari zaidi jipatie nakala yako ya MTANZANIA

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles