23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

JK ajionea adha ya mafuriko Dar

Na Waandishi Wetu, Dar es Salaam

RAIS Jakaya Kikwete jana alitembelea maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam ambayo yameathirika na mafuriko kutokana na mvua inayoendelea kunyesha.

Ziara hiyo ilianzia katika daraja linalotenganisha Mbagala Kuu na Mtoni Kijichi katika Wilaya ya Temeke na kumalizia katika Daraja la Jangwani katika Wilaya ya Ilala.

Rais Kikwete baada ya kuona daraja linalotenganisha Mbagala Kuu na Mtoni Kijichi, alitoa agizo kwa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi Tanzania (JWTZ) kuweka daraja la muda katika eneo hilo huku ujenzi ukiendelea.
Hata hivyo Rais Kikwete alipotembelea katika Daraja la Jangwani aliwataka wahandisi kutumia maarifa kuondoa taka zinazosababisha madaraja hayo kuziba ili maji yaweze kupita kwa urahisi.

“Katika eneo hili tuliwaambia watu wahame lakini walikataa sasa tutafanyaje. Inabidi wahandisi mtumie maarifa ya kutoa taka zilizoziba katika madaraja haya ili maji yasipite juu ya daraja bali yaweze kupita chini kwa urahisi.

“Nimeanza ziara yangu ya kuangalia madhara yaliyotokana na mafuriko na nimeanzia katika eneo la Mbagala na Jangwani.
“Kesho (leo) nitamalizia katika eneo la Mkwajuni na Tegeta na hapo ndipo nitakapotoa hitimisho la athari za mafuriko Dar es Salaam,” alisema Rais Kikwete.

Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Sophia Mjema, alisema imepokelewa msaada wa Sh bilioni 250 kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kutengenenezea daraja la Mbagala Kuu na barabara kwa kiwango cha lami.

Alisema daraja hilo pamoja na barabara vitatengenezwa kwa miezi mitatu hadi minne.

Naye Mhandisi wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Eliseus Mtenga, alisema itatafutwa mashine itakayotoa taka zote zilizoziba katika daraja la Jangwani maji yaweze kupita kwa urahisi.
Habari hii imeandaliwa na Asifiwe George, Ester Mnyika na Mgeni Shabani(EWTC).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles