31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

HANS POPPE HILI LA KAPOMBE UMETELEZA

Na ADAM MKWEPU-DAR ES SALAAM


HUENDA tulimwelewa vibaya Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Simba, Zacharia Hans Poppe, kuhusu Shomari Kapombe, labda kilichotoka mdomoni mwake hakukusudia.

Ni nadra sana kwa kiongozi kama Hans Poppe kumsikia kwenye vyombo vya habari, akimzungumzia mchezaji wake  katika lugha kama ile.Ndio maana hata Katibu Mkuu wa  Simba, Arnold Kashembe, alishanga na kukana huku akisema labda kiongozi mwenzake alinukuliwa vibaya ila haikujulikana hasa kwa faida ya nani.

Hans Poppe aliibuka na kusema beki wao wa kulia Kapombe, anatakiwa kuchagua kucheza au kutocheza, lakini wao hawawezi kuendelea kumlipa mshahara wakati hafanyi kazi anayotakiwa kuifanya.

Poppe amekiri kwamba, walimsajili Kapombe kwa sababu walikuwa wanamhutaji, lakini kama bado hajapona majeruhi yake inabidi wakae na kuzungumza kuona wanafanyaje, kuhusu hilo.

Lakini kumsema Kapombe kwamba majeruhi gani asiyepona muda wote na  kama ni majeruhi basi akae pembeni hadi apone, si busara katika nafasi yake.

Kwani Simba walivyomsajili Kapombe, hawakufahamu kwamba alikuwa na tatizo la majeruhi ya mara kwa mara?

Kwani walimsajili Kapombe wakijua ni yule wa miaka 21 au 25? Hawakufahamu wanamsajili mtu ambaye, anakwenda kumaliza soka lake huko?.

Suala la majeruhi kwa mchezaji ni jambo la kawaida ila Poppe alichotakiwa ni kuzungumza katika lugha ya kistarabu, ili kuondoa ukakasi wa maneno makali aliyotumia, ambayo kwa namna yeyote ile muhusika yatakuwa yamemuumiza.

Kapombe alisajiliwa na Simba, kabla ya kuanza kwa msimu huu baada ya kumaliza mkataba wake na Azam, lakini ameshindwa kucheza mechi yoyote kutokana na kuuguza majeraha aliyoyapata kwenye mchezo wa kwanza wa kuwania kucheza michuano ya CHAN, dhidi ya Rwanda uliochezwa July 15, 2017 Uwanja wa CCM Kirumba Mwanza.

Daktari wa timu ya Taifa, Taifa Stars, Richard Yomba anasema, Kapombe alihitaji uchunguzi kutoka hospitali ya Taifa Muhimbili na hakuwa miongoni mwa wachezaji waliosafiri kwenda Rwanda kwa ajili ya mchezo wa marudiano.

Kapombe yupo kwenye matibabu ya awali ya saa 72, kutokana na hali yake ya sasa hatoweza kushiriki mazoezi na wenzake. Inatakiwa kuwa na moyo wa aina ya Poppe ili kukubaliana naye kwamba Kapombe amegoma kucheza kwa sababu anaogopa kuhumia tena, hii haingii akilini ata kidogo.

Viongozi lazima wawe na lugha ya kuongoza ila si ya vijiweni, kama ambavyo Poppe ameitumia katika kulielezea suala la Kapombe.Inasikitisha.

Mara ngapi tunashuhudia wachezaji wa aina ya Kapombe katika klabu nyingine na bado viongozi wa klabu hizo wanatumia busara katika kumaliza tatizo, baadae wanaachana na mchezaji bila maneno ya kuudhi ambayo yanakatisha tamaa wachezaji wengine?.

Binafsi sikubaliana na Poppe kwa maneno aliyotumia, hayakubaliki katika tasnia ya mchezo huu maana si tabia yetu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles