23.1 C
Dar es Salaam
Sunday, September 8, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Biteko ampongeza Mavunde kwa Teachers Breakfast Meeting 2024 Dodoma

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Madini, Dk. Doto Biteko amewataka walimu wa shule za Msingi na Sekondari jijini Dodoma kumuunga mkono Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini, Antony Mavunde kwa kufanyakazi kwa bidii kwa kuhakikisha wanaongeza ufaulu katika Jiji hilo.

Kauli hiyo ameitoa leo Jumamosi Juni 1,2024 wakati akizungumza na walimu wa shule za msingi na sekondari Jijini Dodoma katika Mkutano uliopewa jina la ‘Teachers Breakfast Meeting 2024.

Mkutano huo uliandaliwa na Mavunde ambaye pia ni Waziri wa Madini na ulihudhuriwa na Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri, Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, John Kayombo na waratibu wa elimu.

Dk. Biteko amesema Mavunde amekuwa kinara wa kuhakikisha Jimbo la Dodoma Mjini linafanya vizuri katika sekta ya elimu hivyo walimu wana wajibu wa kuhakikisha wanamsaidia kwa wanafunzi kufaulu.

“Kila mmoja anaona dhamira ya Mheshimiwa Mavunde katika sekta ya elimu,walimu niwaombe jitahidini wanafunzi waweze kufaulu kwani amekuwa akijitoa kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora na katika mazingira sahihi,” amesema Dk. Biteko.

Aidha, Dk. Biteko amesema mtu wa kwanza anaeweza kumtengeneza mtoto ni mwalimu hivyo wana wajibu wa kumtengeneza ili awe bora.

“Walimu mnayo kazi kubwa ya kututengenezea Taifa kwa kutafsiri R4 za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan hasa kwenye suala la maridhiano,” amesema Dk. Biteko.

Dk. Biteko amesema Mataifa yote yaliyoendelea uwekezanj wake upo katika elimu na ndiko alikowekeza Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake Mavunde amesema lengo la Mkutano huo ni kujadili changamoto wanazokutana nazo walimu katika muhula uliopita na wafanye nini katika muhula ujao ili kuendelea kuwatia moyo.

“Tuliona njia pekee ya kufanya vizuri ni kuwaweka walimu pamoja hatutaki mwalimu wetu akiwa na changamoto akalalamike sehemu nyingine kwani haya ni sehemu ya maisha yetu,” amesema Mavunde

Amesema kupitia mkutano huo watazungumza kwa pamoja na kuweka utaratibu mzuri wa kutatua kero ambazo zitajitokeza.

“Dhamira yangu ni ya dhati katika kukuza elimu kwani nimeweza kujenga shule za msingi na sekondari kwa wanafunzi waliokuwa wakitembea umbali mrefu,”amesema Waziri Mavunde.

Amesema kwa kushirikiana na baadhi ya wadau wameweza kujenga uzio katika shule mbalimbali ambao unasaidia watoto kusoma kwa utulivu.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema Mbunge wa Dodoma, Anthony Mavunde anathamini elimu na kila anapokutana nae huwa anahoji kuhusu miradi mbalimbali ya elimu katika Jimbo la Dodoma Mjini.

Prof. Mkenda amesema kwenye miundombinu Rais Samia Suluhu Hassan wamejenga Vyuo vya Ufundi (Veta) 64 kwa mkupuo na Campus katika Vyuo Vikuu vyote katika maeneo mbalimbali.

“Tunapoenda kila Mkoa kutakuwa na Campus ya Chuo Kikuu lengo letu ni kuhakikisha elimu inakuwa karibu na wanafunzi,”amesema Prof. Mkenda.

Aidha, Prof. Mkenda amesema kuna mageuzi makubwa katika sekta ya elimu.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule.
- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles