25.1 C
Dar es Salaam
Monday, October 28, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Biteko aitaka TANESCO kutatua changamoto ya umeme Lindi/Mtwara

Na Mwandishi wetu, Mtwara

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko amelitaka Shirika la Umeme nchini (TANESCO),kuja na suluhisho la changamoto ya umeme Lindi/Mtwara inayohitaji megawati 22, pekee.

Waziri huyo ambaye amemaliza ziara ya kikazi ya siku tatu katika mikoa hiyo, amesema Serikali inaiangalia menejimenti ya TANESCO lakini kwa sasa ijitathmini na ijikite kwenye kupelekea watu umeme.

Ameitaka TANESCO Makao Makuu kuacha kujirundikia majukumu ikiwemo ya manunuzi ambayo yanarudisha nyuma shughuli za shirika na kuleta urasimu.

Kuhusu kero ya upatikanaji wa umeme wa uhakika katika Kisiwa cha Songosongo, Dk. Biteko ameagiza, umeme unaoendesha mitambo ya TPDC na PAN AFRICAN ENERGY uende pia kwa wananchi wa kisiwa hicho.

Amemuagiza na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kwenda Songosongo Novemba 18,2023 ili kuanza hatua za kusambaza umeme kwa wananchi takriban 5000.

“Nikianzia Songosongo ambapo gesi inatoka, wananchi pale wana malalamiko yote ya msingi, mfano kuna watu walikuwa wakifanya kazi za ulinzi katika mitambo na visima vya gesi, pesa yao hawajalipwa kwa miaka kadhaa sasa.

“Hivyo madai haya TPDC na Songas mtayalipa, Serikali ya Awamu ya Sita hataivumilia kuona jambo hili linafanyika, TPDC hakikisha ndani ya mwezi wa Disemba, hawa watu wote wawe wamelipwa pesa zao,”amesema Dk. Biteko.

Pia ameiagiza TPDC kwa kushirikiana na kampuni ya PAN AFRICAN ENERGY na SONGAS kutafuta kivuko na kukipeleka kwenye kisiwa hicho ili kiwasaidie wananchi.

Akizungumzia malalamiko ya Wananchi katika kijiji cha Msimbati na Madimba wilayani Mtwara, ameitaka TPDC kujenga kituo cha afya katika moja ya vijiji ili wananchi wafaidi matunda ya kuwepo kwa mradi wa gesi.

Ameitaka pia kukarabati kituo cha Polisi na kuweka taa za barabarani ndani ya mwezi Disemba.

Hata hivyo ameipongeza TPDC kwa majukumu inayofanya na kuitaka kuja mpango wa muda mrefu wa upatikanaji wa gesi asilia na mafuta.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
591,000SubscribersSubscribe

Latest Articles