Amina Omari, Korogwe
Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Kissa Bwakisa, ametoa msaada wa mbao vipande 100 vyenye thamani ya zaidi ya sh milioni 1.6 kwa Shirika la Maendeleo la Brac kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa matundu ya vyoo 20 katika utekelezaji wa mradi wa elimu wilayani humo.
Akikabidhi msaada huo kwa viongozi wa shirika hilo leo, Bwakisa amesema kuwa lengo ni kusaidia kuboresha miundombinu ya kielimu.
“Tunajua kwamba Brac wanatusaidia kuwaanda watoto wetu katika kupata elimu hivyo nimeona niwaunge mkono kama wadau wa maendeleo kwani baada ya mradi kumaliza majengo yatabaki chini ya serikali” amesema.
Kwa upande wake Meneja Mawasiliano wa Brac Tanzania, Emma Mbaga, amesema mradi wa elimu nje ya mfumo rasmi umeweza kujumuishwa jumla ya mabinti zaidi ya 300 na watoto chini ya umri wa miaka saba zaidi ya 200.
Hata hivyo Afisa Elimu ya watu wazima na mfumo usiorasmi Asseri Mshana, amesema kuwa mradi huo umehusisha ujenzi wa madarasa 12 pamoja na matundu ya vyoo 20 jumla ya thamani ya sh milioni 95.