25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

DAWASCO ITOKE PWANI ILI MKOA UJITEGEMEE KWA MAJI

Na Shermarx  Ngahemera  

MAJI yanayotumika Dar es Salaam yanatoka Mkoa wa Pwani na katika mazingira tegemezi maji hayo  yamehodhiwa na Dar es Salaam, kutokana na uchumi wake kuwa mkubwa na hivyo kuinyonya Pwani, mkoa ulio jirani na  sasa unaochipukia kwa kasi kiuchumi.

Mkoa wa Pwani kwa miaka mingi umekuwa tegemezi kwa miundombinu yake kutokea Dar es Salaam na kuacha kushughulikia matatizo yake na hivyo kusinyaa kiuchumi hadi Awamu  hii ya  Tano ya Utawala .

Wajuzi  wanasema hakuna marefu yasiyo na ncha na kwa hali ilivyo inabidi Pwani ijitoe kwenye kumilikiwa na Dar es Salaam kama inataka maendeleo ya haraka na ya kuaminika  ya uchumi wake.

Kunaonekana kuna mgongano wa masilahi wa wazi  umeanza kujitokeza katika rasilimali za msingi ikiwamo maji, ambapo  Pwani inaonekana kutoridhika na mambo yanavyokwenda kwani kipaumbele hutolewa kwa Dar es Salaam badala ya Pwani mwenye maji yake kwani yanazalishwa kwenye mkoa wake.

Kuzingatia ukweli wa hali hiyo inayokosesha afya ya kiuchumi, Serikali imeitaka bila kumung’unya maneno Shirika Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasco) kushiriki katika mfumo wa uchumi wa viwanda katika Mkoa wa Pwani.

Pia, wametakiwa kuhakikisha mkoa huo unapata maji safi na salama ili wawekezaji waweze kujenga viwanda haraka na kwa  ufanisi zaidi.

Kwa maelezo ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage, kuna  viwanda zaidi ya 300 mkoani Pwani ambavyo viko katika hatua mbalimbali za ujenzi mkoani Pwani na vitaanza  kufanya kazi karibuni.

Kinachogomba ni kuwa Dawasco kama jina lake linavyoonesha limejikita zaidi kiutendaji kwa Dar es Salaam kama jiji na mkoa na hivyo maendeleo yanayofanyika  mkoani Pwani si kipaumbele chake  isipokuwa Bagamoyo ambayo inayo uhusiano wa kihistoria na kitamaduni na hivyo kuhusishwa katika picha kubwa  ya mipango ya maji.

Wilaya nyingine mkoani Pwani zikiwamo za Rufiji, Kibiti, Kisarawe na Mkuranga hakuna maji ya Dawasco na hivyo kudai uundwaji wa kampuni mpya ya maji kwa mkoa wa Pwani ili kufikisha huduma hiyo kwa viwanda vinavyokuja kwa  nguvu kubwa na kwa wakazi wa mkoa huo. Wakazi hao wanataka vilevile chanzo cha maji kibadilike na kuwa Mto Rufiji badala ya Mto Ruvu.

Ukweli unaonesha Dawasco haina uwezo wa kuhudumia  Mkoa wa Pwani kwani Dar es Salaam yenyewe inawashinda  kwa viwango vya hivi sasa.

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandidi  Isaack Kamwelwe, akizungumza wakati wa uzinduzi wa bodi ya tano ya wakurugenzi wa Dawasco Kibaha mkoani Pwani, alisema maji yamekuwa chanzo kikubwa kwa wawekezaji kushindwa kuwekeza kwenye  viwanda kikamilifu mkoani humo.

Mhandisi Kamwelwe  alilalama  kuona  hali mbaya ya  maji Mkoa wa Pwani na kusema Kisarawe kuna mradi mkubwa wa viwanda, lakini unashindwa kuendelea kwa sababu ya kukosa huduma hiyo ya maji, lakini hakutoa suluhisho lake  kwani yeye ni mhusika mkuu wa tatizo.

Alisema Juni 21, mwaka huu, Rais Dk. John Magufuli  akiwa Kibaha, Pwani, alishatoa agizo mkoani humo kupelekwe maji safi ili shughuli za ujenzi wa viwanda uendelee.

Kamwelwe aliitaka Kampuni ya Dawasco ifikapo mwaka 2020, Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam iwe imefikia asilimia 95 ya upatikanaji wa maji safi na salama. Wakazi wanasema muda huo ni mbali sana na kudai leo.

Waziri Kamwele  alikumbushia  na kushangaa kuwa  rais alishatoa agizo kupelekwa kwa miundombinu ya maji  Mkoa wa Pwani, inashangaza mpaka hivi sasa kuna sehemu nyingine bado miundombinu haijafika, hali hiyo inasababisha kukosa wawekezaji.

Kwa mtazamo wa mambo, wachunguzi wanasema si rahisi Dawasco kufikiria kwa undani suala la  kupeleka maji Mkoa wa Pwani, kwani wana kasumba kuwa wao kama wanavyosomeka  ni kwa ajili ya Dar es Salaam na si Kibaha na hivyo kupeleka  maji Kibaha ni hisani na si kipaumbele kama inavyotakikana.

Ukweli wa mambo ni kuwa mpanda ngazi  na mshuka ngazi hawawezi  kushikana mikono kwani ni lazima waachane  ikiwa wanataka kupiga hatua.  Kwani mkoa wa Pwani unapanda ngazi na Da re sa Salaam inashuka na hata kunyag’anywa  Makao Makuu ya Serikali kwani yanahamia Dodoma.

“Mkoa wa Pwani ndio unaongoza kwa miradi mipya ya viwanda ambapo hivi sasa kuna viwanda 82, hivyo ni muhimu miundombinu ya maji iboreshwe ili viwanda vifanye kazi kwa uharaka ili kukuza uchumi kwa Taifa,” alisema Mhandisi  Evarist Ndikilo ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani.

Anathibitisha Mkuu wa Mkoa  huyo kuwa bado kuna changamoto ya maji katika Mkoa wa Pwani, ingawa kwa mahitaji ya sasa upatikanaji maji  umefikia asilimia 62.5 ya mahitaji na hivyo Dawasco wanahitajika kuongeza nguvu zaidi ili kufanikisha uchumi wa viwanda nchini.

Mahitaji ya maji yanajitokeza katika sura mbalimbali kama kipoza, malighafi na matumizi ya usafi viwandani.  Wajuzi wanasema hakuna kiwanda bila maji na hivyo Dawasco wawe wakweli na waache kung’anga’ania wasichokiweza.

Kaluwa  Steel Mills  Mlandizi nao  walilazimika kuvuta umeme  kilomita 4 toka ‘substation’ na kiwanda kama  Twyfords  Tiles  wametafuta suluhisho lake kwa  kuvuta wenyewe maji toka Mto Ruvu wakati wakisubiri upatikanaji mwafaka wa maji toka Dawasco, wakati kiwanda cha Goodwill Tanzania Ceramics kilichopo Mkuranga kina mahitaji makubwa ya maji kwani kinaanza  uzalishaji mapema mwakani.

Lawama hizo zinamfanya Mkurugenzi wa Dawasco, Cyprian Luhemeja, asipate usingizi  na kusema  kuwa upatikanaji wa maji umeongezeka kwa asilimia 75 wakati upotevu wa maji umepungua kwa asilimia 28. Awali upotevu wa maji  kutokana na wizi  na  mtandao uliochakaa ulifikia kiwango cha kutisha cha asilimia 40. Anasema Bagamoyo iko kwenye mradi mkubwa  wa maji unaotekelezwa na kampuni ya Kihindi.

Alisema malengo waliojiwekea Dawasco ni kuwa ifikapo 2020, asilimia 95 ya upatikanaji wa maji itakuwa imeboreshwa na ifikapo mwaka 2025 watu milioni 10 wanatakiwa kupata maji safi na salama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles