24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

CUF yanyakua kiti cha Zitto, PAC

Amina MwidauNa Mwandishi Wetu, Dodoma
WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, wamemchagua Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mwidau (CUF) kuwa mwenyekiti wa kamati hiyo.
Katika uchaguzi uliofanyika jana mjini hapa, Mwidau alichaguliwa na wajumbe wa PAC kwa kupata kura 15 dhidi ya mpinzani wake, Lucy Owenya (Chadema) aliyeambulia kura mbili.
Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa nafasi hiyo, Mwidau alisema atafanya kazi iliyoachwa na Zitto Kabwe wakati akiiongoza kamati hiyo kwa kuzingatia masilahi ya nchi na siyo watu binafsi.
“Moto ni uleule ambao umeachwa na mwenyekiti mtangulizi wangu, Zitto Kabwe, na tutafanya kazi pale alipoishia maana nikiwa mjumbe wa kamati hii tulifanya kazi kama ndugu wa familia moja.
“Zitto na Deo Filikunjombe waliweka misingi imara katika PAC na hilo tutaendelea nalo na tutafanya kazi kama jicho la Bunge kwa Serikali hasa katika kusimamia na kulinda rasilimali za Watanzania ila tunawaomba waendelee kutuamini,” alisema Mwidau.
Alisema ingawa imebaki takribani miezi minne Bunge kuvunjwa, kamati yake itaendelea na ratiba yake ya mwaka iliyokuwa imepangwa.
“Kama mwenyekiti kazi yangu kubwa ni kuiongoza kamati kwa mujibu wa taratibu, sisi tunakagua hesabu za serikali kuu na mashrika ya umma.
Tunaangalia namna serikali inavyofanya kazi yake, tuna mpango wa kazi, ratiba ya mwaka mzima tutaendelea nayo,” alisema.
Alisema pia kuwa kamati itaendelea na msimamo wa uwajibikaji na uwazi ambao ulikuwa ukisimamiwa na Zitto.
Akizungumzia kuchaguliwa kwa Mwidau kuongoza Kamati hiyo, Mwenyekiti wa zamani wa PAC, Zitto Kabwe alimpongeza kwa kushinda nafasi hiyo akisema ana imani ataendelea kusimamia mifumo ya uwajibikaji.
“Nampongeza kwa dhati dada yangu kwa imani aliyopewa na wajumbe wenzake wa PAC. Nimefanya kazi na Amina tangu mwaka 2010 tulipokuwa Kamati ya POAC na nina imani kwa ushirikiano mkubwa wa Makamu Mwenyekiti Deo Filikunjombe wataendeleza kazi tuliyoianza ya kujenga mfumo madhubuti wa uwajibikaji nchini kwetu,” alisema Zitto.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles