24 C
Dar es Salaam
Wednesday, May 8, 2024

Contact us: [email protected]

ACT Wazalendo yaanza kukusanya maoni kuhusu Tume Huru ya Uchaguzi

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Katibu Mkuu wa ACT Wazalendo, Ado Shaibu amesema kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Chama cha ACT Wazalendo imeagizwa kuanza mchakato wa kukusanya maoni ya Wanachama kuhusu Tume Huru ya Uchaguzi inayotakiwa na ACT Wazalendo.

Shaibu ameyasema hayo Desemba 21, wakati akizungumza na viongozi wa ACT Wazalendo katika Jimbo la Nyasa mkoani Ruvuma katika mwendelezo wa ziara yake kwenye mikoa ya Ruvuma, Selous, Mtwara, Lindi, Pwani na Tanga.

Lengo la ziara hiyo ni kujenga Chama, kuhamasisha na kufanya harambee ya michango ya wanachama ya kugharamia Mkutano Mkuu wa Chama wa Januari 29, 2022 na kufafanua mageuzi ya uendeshaji Chama kisayansi yanayotarajiwa kuzinduliwa kwenye Mkutano Mkuu huo.

“Kwenye kikao cha Wadau wa Siasa juu ya Hali ya Demokrasia nchini kilichofanyika Dodoma, suala la Tume Huru ya Uchaguzi liliafikiwa na pande zote. Kwetu sisi ACT Wazalendo, hatua inayofuata ni mjadala wa kitaifa kuhusu aina ya Tume Huru tunayoihitaji,” amesema Shaibu.

Kiongozi huyo amesema kuwa vikao vya ACT Wazalendo (Kamati Kuu ya mwezi Juni na Halmashauri Kuu ya mwezi Oktoba 2021) vimeagiza Chama kulipa kipaumbele suala la Tume Huru ya Uchaguzi.

Shaibu amesema kuwa mbali na maoni ya wanachama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa ACT Wazalendo imeagizwa kufanya rejea ya uzoefu wa nchi nyingine zenye mifano ya Tume za Uchaguzi zinazopigiwa mfano pamoja na Ripoti na Taarifa mbalimbali ikiwemo Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba.

Aidha, amewaeleza viongozi wa Chama jimboni Nyasa kuwa Chama kitaendelea kulipa kipaumbele suala la Tume Huru ya Uchaguzi ili chaguzi za mwaka 2024 (Serikali za Mitaa) na 2025 (Uchaguzi Mkuu) ziwe huru, za haki na zenye kuaminika.

Kiongozi huyo anaendelea na ziara yake mkoani Ruvuma.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles