24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

ACT-Tanzania vipande vipande

 

Pg 2

SHABANI MATUTU NA JUMA HEZRON, DAR ES SALAAM
NI wazi sasa hali ya mambo ndani ya Chama cha Alliance for Change and Transparency (ACT-Tanzania) si shwari kutokana na chama hicho kuwa vipande vipande.
Hali hiyo imetokana na wajumbe wa Kamati Kuu kupiga kura ya kutokuwa na imani na Mwenyekiti wa muda wa chama hicho, Kadawi Limbu ambaye Desemba 30, mwaka jana, alitangaza kuwafukuza uanachama Katibu Mkuu wa muda, Samson Mwigamba, mshauri wa chama hicho, Profesa Kitila Mkumbo na wajumbe wengine wanane.
Wajumbe hao kwa kauli moja, waliazimia kumsimamisha Naibu Katibu Mkuu (Bara), Leopold Mahona na Mwenyekiti wa muda wa Ngome ya Vijana, Grayson Nyakarungu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwanasheria Mkuu wa chama hicho, Thomas Matatizo, alisema Kamati Kuu imefikia uamuzi wa kumwondoa Limbu katika nafasi yake baada ya kujiridhisha kuwa amepoteza sifa za msingi za kuongoza chama.
“Kwa kuwa Kamati Kuu haishughuliki na nidhamu kwa ngazi ya mwenyekiti wa taifa, tumependekeza Halmashauri Kuu ya Taifa ichukue hatua stahiki za kinidhamu dhidi yake,” alisema.
Akizungumzia suala la Mahona, alisema kikao hicho kilimsimamisha kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho Ibara ya 27(c) na wamemtaka aendelee kusubiri hatua ya uamuzi wa Halmashauri Kuu ambayo ndiyo mamlaka iliyomteua.
Alisema kwa upande wa Nyakarungu, ameachishwa kazi kwa mujibu wa Katiba ibara ya 37(n){xxii}, kwa kosa la kukataa kutumikia nafasi yake ya mwenyekiti wa muda wa Ngome ya Vijana nafasi aliyoteuliwa na Halmashauri Kuu ya Taifa.
Alisema Kamati Kuu imeunda kamati maalumu ya nidhamu kwa ajili ya kushughulikia tuhuma mbalimbali dhidi ya Nyakarungu, Mahona na Limbu.
“Kamati hii imeagizwa kukamilisha kazi yake ndani ya siku saba tangu walipokabidhiwa jukumu hili na kuwasilisha mapendekezo kwenye kikao cha Halmashauri Kuu,” alisema.
Alisema uamuzi wa Limbu kuwafukuza Mwigamba na Profesa Kitila katika chama hicho ulikuwa batili kwa sababu haukuzingatia Katiba, sheria na utaratibu.
Akizungumzia vurugu zilizotokea, Mwigamba alisema zinachangiwa na mahasimu wa kisiasa wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) ambaye anatajwa kuonyesha nia ya kujiunga na chama hicho.
Alisema sababu nyingine inatokana na wapinzani wao wa kisiasa wanaotaka kuona chama hicho kinasambaratika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles