28.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

JK afichua kipigo cha Lipumba

kkNa Fredy Azzah

SIKU chache baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba na wafuasi wake kupigwa na polisi, Rais Jakaya Kikwete amesema tukio hilo limetokea kwa sababu nchi inaongozwa kwa sheria na atakayekiuka atakumbana na mkono wa sheria.
Rais Kikwete alitoa kauli hiyo jana Ikulu jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kufanya mazungumzo ya faragha na mgeni wake, Rais wa Ujerumani, Joachim Gauck, ambaye yuko nchini kwa ziara ya siku tano.
Kabla ya Rais Kikwete kutoa kauli hiyo, Rais Gauck aliimwagia sifa Tanzania kutokana na namna inavyofuata utawala wa sheria, uhuru wa vyombo vya habari na kulinda haki za binadamu.
Baada ya viongozi hao kuzungumza mbele ya waandishi wa habari juu ya ziara hiyo, waandishi walipewa fursa ya kuuliza maswali na ndipo mmoja wa wanahabari kutoka Ujerumani, alipotaka kauli ya Rais Kikwete na Rais Gauck, juu ya msingi wa uhuru wa vyombo vya habari na haki za binadamu nchini, wakati hivi karibuni gazeti la The East African lilifungiwa na wanachama wa CUF kupigwa na polisi walipotaka kuandamana.
Akijibu swali hilo, Rais Kikwete alisema: “Tuna sheria zinazoongoza mambo hayo, huwezi kuamka tu ukaamua kuandamana, tuna taratibu zetu za vyama vya siasa kukusanyika, wala hatubani haki na uhuru wa wapinzani, ukivunja sheria hiyo utawajibishwa.
“Na hapa wapinzani ndio wanafanya mikutano mingi kuliko chama tawala, ikitokea hawajafuata taratibu, hatuwezi kuwaacha waendelee kuvunja sheria,” alisema Rais Kikwete.
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Profesa Lipumba alisema walifuata sheria zote na pia kutii amri ya polisi ya kuwataka kuacha kuandamana na kufanya mkutano wa hadhara.
CUF walipanga kuandamana na kufanya mkutano wa hadhara kukumbuka wenzao waliouawa mwaka 2001.
Kuhusu kufungiwa kwa gazeti la kila wiki la The East African linalochapishwa nchini Kenya na Kampuni ya Nation Media Group (NMG) na kusambazwa Tanzania, Rais Kikwete alisema halijafungiwa bali lilibainika kusambazwa nchini bila kuwa na kibali.
Alisema baada ya kubainika hilo, kampuni inayochapisha gazeti hilo ilitakiwa kutoendelea kulisambaza nchini hadi kibali cha kufanya hivyo kitakapopatikana.
Rais Kikwete alisema kwa sasa utaratibu wa kutoa kibali hicho unaendelea.
Alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache duniani ambazo zinajali uhuru wa vyombo vya habari, na hata sasa kuna magazeti mengi yaliyosajiliwa na yanachapishwa kila siku.
Akizungumzia kuhusu hali ya usalama na tishio la ugaidi, Rais Kikwete alisema hawezi kusema kuwa Tanzania iko salama asilimia 100, lakini kutokana na hatua zinazochukuliwa za kulinda amani na usalama, hali iko shwari.
“Tunashirikiana vizuri na vyombo vya usalama vya kimataifa, tunadabilishana taarifa kila inapobidi, siwezi kusema kuwa sisi tuko salama kwa asilimia 100, kwamba hatuwezi kuguswa kutokana na mikakati ya kulinda amani, hali kwetu ipo shwari,” alisema.
Katika hatua nyingine, aliiomba Ujerumani kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini, ikiwamo gesi, viwanda na biashara.
Alisema Tanzania baada ya kugundua gesi asilia, pamoja na mambo mengine itatumika kwa matumizi ya nyumbani kwani kwa sasa zaidi ya tani 40 za mkaa hutumika Dar es Salaam pekee kila mwaka, hivyo kiasi kikubwa cha miti huteketea.
Kwa upande wake, Rais Gauck, alisema Ujerumani iko tayari kuendeleza ushirikiano wa kisiasa na kiuchumi na Tanzania na ndiyo maana katika msafara wake ameongozana na wadau mbalimbali wa sekta za kiuchumi, wakiwamo wafanyabiashara wakubwa na waziri husika kwa lengo la kujifunza na kuangalia fursa za uwekezaji.
Alisema anaridhishwa na jinsi Tanzania inavyosimamia haki za binadamu na kasi ya kushughulikia tatizo la rushwa, umoja wa kitaifa na maendeleo,
na kwamba Ujerumani itaendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za maendeleo na Tanzania.
Rais Gauck alisema nchi hizi mbili zimekuwa na ushirikiano wa kihistoria tangu mwaka 1961, na ndiyo maana kuna miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii iliyotekelezwa, na kwamba Ujerumani inaisaidia kiuchumi Tanzania.
Aliipongeza pia Tanzania kutokana na kushiriki katika kutuliza migogoro ya kikanda, ikiwa ni pamoja na kutafuta amani Sudan Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Alisema Tanzania ni mfano wa kuigwa kwa jinsi inavyojituma kupeleka majeshi yake katika mataifa yenye machafuko, kwani kwa kufanya hivyo inajilinda yenyewe.
Rais Gauck anatarajiwa pia kutembelea Zanzibar, Bagamoyo, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na ameomba akae Arusha kwa muda kabla ya kurejea Ujerumani, kwani mji huo una sifa ya kipekee duniani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles