27.2 C
Dar es Salaam
Friday, September 20, 2024

Contact us: [email protected]

Wizara nne kushughulikia vyanzo ukatili kwa watoto

Na Nora Damian, Mtanzania Digital

Serikali inatarajia kuunda kamati maalumu itakayohusisha Wizara ya Katiba na Sheria, Mambo ya Ndani ya Nchi, Maendeleo ya Jamii na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kubaini vyanzo vya ongezeko la ukatili kwa watoto nchini.

Akizungumza leo Juni 5,2024 wakati wa kongamano la kujadili utumikishwaji wa watoto Waziri wa Sheria na Katiba, Dk. Pindi Chana, amesema kamati hiyo itahusisha Wizara ya Mambo ya Ndani, Tamisemi, Maendeleo ya Jamii ili kuweka mikakati zaidi ya ulinzi wa watoto na kudhibiti vitendo vya ukatili.

Waziri wa Sheria na Katiba, Dk. Pindi Chana, akizungumza wakati wa kongamano la kujadili utumikishwaji wa watoto.

Kongamano hilo limeandaliwa kwa ushirikiano na Mtandao wa Kupinga Utumikishwaji wa Watoto na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika inayoadhimishwa Juni 16 kila mwaka.

“Tumekubaliana tukutane tuweke mikakati ya kuangalia vyanzo vya ukatili kwa watoto, tutashirikiana na familia, shule, taasisi za dini ili tuweze kudhibiti ukatili.

Mratibu wa Mtandao wa Kupinga Utumikishwaji wa Watoto nchini, Scholastica Pembe, akizungumza wakati wa kongamano la kujadili utumikishwaji wa watoto.

“Sote tunapaswa kuwa mabalozi wa walinzi wa watoto, kuna baadhi ya watu wanawatumikisha watoto, ukiona, ukisikia usisite kutoa taarifa,” amesema Dk. Chana.

Amesema Tanzania ni mwanachama wa mikataba mingi ya kimataifa hususan ya kumlinda mtoto hivyo wakati umefika wa kuweka mikakati kuhakikisha mtoto anapata haki zake ikiwemo ya elimu, matibabu na kulindwa dhidi ya utumikishwaji na shughuli nyingine.

Waziri hiyo amesema pia wanaendelea kufanya maboresho ya sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Mtoto kuhakikisha mtoto analindwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la UN Global Compact Chapa ya Tanzania, Marsha Yambi, amesema watoto milioni 200 wanatumikishwa katika kazi mbalimbali duniani ambapo kati yao milioni 73 wako chini ya miaka 10.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo kilimo kinaongoza kwa kuajiri watoto wengi hasa katika mashamba ya chai, tumbaku, miwa, mwani, karafuu na shughuli za uvuvi.

“Sekta binafsi inaonekana inachangia kuajiri watoto wadogo kwenye mashamba, tuhakikishe watoto hawawi katika ajira na tupate faida kwa haki na siyo kwa kupitia watoto,” amesema Yambi.

Mratibu wa Mtandao wa Kupinga Utumikishwaji wa Watoto nchini, Scholastica Pembe, amesema kongamano hilo linalenga kujadili sera na sheria zinazomlinda mtoto na kutolea mfano Sheria ya Ndoa ambayo inaruhusu mtoto aolewe chini ya miaka 18.

Amesema pia Sheria ya Kazi inaruhusu mtoto aanze kufanya kazi kuanzia miaka 14 na kuendelea lakini afanyishwe kazi ambazo si hatarishi na apate muda wa kucheza.

“Unaweza kujiuliza mtoto ambaye pia ni mama anapata wapi muda wa kucheza, muda wa kupumzika na asifanye kazi hatarishi ambazo ni pamoja na kuingia jikoni. Kwahiyo bado tunalo jukumu la kuangalia sera na sheria zetu zimekaaje ili kumlinda mtoto,” amesema Pembe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles