25.2 C
Dar es Salaam
Saturday, September 21, 2024

Contact us: [email protected]

MAHAKAMA YAAMURU NG’OMBE 1,300 WAPIGWE MNADA

NA OMARY MLEKWA-MWANGA

MAHAKAMA ya Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro imeamuru ng’ombe 1,325 waliokamatwa katika operesheni ya kukamata mifugo inayoingizwa nchini kinyume na taratibu  kwa ajili ya malisho, kupigwa  mnada Oktoba 20, mwaka huu.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina alisema licha ya mifugo hiyo kuingizwa nchini pia  imechangia uharibifu wa mazingira, kukauka vyanzo vya maji, uharibifu wa misitu na  mmomonyoko wa udongo.

Aliyasema hayo alipotembelea eneo la Kata ya Mgagao walipohifadhiwa ng’ombe hao

Mpina  alisema  operesheni inayoendelea ya kusaka  mifugo iliyoingia nchini kinyume cha sheria isihusishwe na ushirikiano  mwema uliopo baina ya Tanzania na nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika  Mashariki.

“Mahakama  imeiteua na kutoa idhini kwa  Kampuni ya Maripelanto Auctioneer & Court Broker ya Moshi  kusimamia  uuzwaji wa ng’ombe   hao keshokutwa  ikiwa ni utekelezaji wa agizo alilolitoa wiki iliyopita la kutaka  mifugo hiyo itaifishwe.

“Tunafanya operesheni hiyo ya kwanza na ya  mwisho kwa sababu  haiwezekani makundi makubwa ya mifugo yakaingia nchini  wakati maeneo hayo wapo watumishi wa Serikali.

“Hivyo ni dhahiri  kutakuwa na uwajibikaji hafifu wa watumishi hao na kamwe Serikali ya  awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli haitawavumilia  watumishi wa aina hiyo,” alisema Mpina.

Alisema muda wa siku saba aliotoa wa mifugo kuondolewa nchini  umekwisha na ataongoza operesheni nchi nzima itakayochukua siku  15 kuhakikisha hakuna mfugo hata mmoja utakaobaki kutoka nchi  jirani.

“Tanzania haiwezi kuwa mahali pa kulisha mifugo kutoka  nchi jirani huku wafugaji wazawa wakiendelea kuteseka kwa kukosa  malisho.

“Inakadiriwa kuwa  asilimia 30 ya malisho yanatumiwa na  mifugo kutoka nje ya nchi ambako Sheria ya Mifugo Namba 17  ya Mwaka  2003 inakataza mifugo kuingia nchini bila kibali,” alisema .

Waziri alisema hatua hizo kali anazozichukua sasa zimelenga  kuwakinga wafugaji wazawa na magonjwa ya mifugo kutoka nje ya nchi  kwa sababu  ikiwa hali hiyo itaendelea ng’ombe wengi watakufa huku Serikali  ikilazimika kutumia gharama kubwa kutibu mifugo hiyo.

Mpina amewaagiza wakuu wote wa mikoa na wilaya za mikoa ya  Arusha, Kilimanjaro, Mara, Kagera, Tanga, Songwe, Mbeya, Katavi,  Njombe, Kigoma kusimamia hatua hiyo ya mifugo kurudishwa nchi  zilikotoka.

Alisema hicho ndicho kitakuwa kipimo cha viongozi hao katika kusimamia shughuli za Serikali.

“Katibu Mkuu wa wizara  na maofisa mifugo kote nchini  hakikisheni mnasimamia kwa ukamilifu sheria na katika kipindi hiki cha  mimi kuwa waziri wa wizara hii na Serikali ya awamu ya tano hatimaye mifugo na mazao yake viweze kuleta tija kwa  Taifa,”alisema Mpina.

Mambo ya Nje wanena

Wizara ya Mambo ya Nje Na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imetoa tamko na la uingizaji mifugo kutoka nchi moja kwenda nyingine ikisema una madhara mengi, yakiwamo ya usalama, uharibifu wa mazingira na kueneza magonjwa ya mifugo.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa Oktoba 13, mwaka huu Wizara ya Mifugo na Uvuvi ilitoa agizo la kuondoa mifugo yote iliyopo nchini kinyume cha sheria ndani ya siku saba na kutofanya hivyo kutasababisha  mifugo hiyo kutaifishwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

“Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inatoa wito kwa Watanzania wote wenye mifugo nchi jirani wafuate taratibu za sheria na kama kuna mifugo kwenye malisho nje ya Tanzania waiondoe mara moja kuepusha hasara na usumbufu,” ilieleza taarifa hiyo

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles