31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Zitto: Nitachukua uamuzi mgumu

Zitto_Kabwe_2011Na Freddy Azzah, Kigoma

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ametua jimboni kwake na kuomba kuungwa mkono kwa hatua yoyote atakayochukua kuanzia sasa.

Kauli hiyo aliitoa mjini hapa jana, alipokuwa katika kikao cha ndani na viongozi wa jimbo hilo.

Ingawa hakuweka wazi ni hatua gani atakayochukua, lakini wachambuzi wa siasa wanasema pengine atachukua uamuzi mgumu kutokana na matukio kadhaa yaliyomtokea katika maisha yake ya kisiasa.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa na takriban watu 250, wakiwamo wawakilishi wa wazee, vijana na wanawake, huku wakiwa wamevaa fulana yenye picha ya Zitto zenye maandishi yaliyosema ‘Miaka 10 ya utumishi Kigoma’, alisema hakuna kiongozi mkubwa wa kisiasa duniani ambaye hajawahi kupigwa vita.

Alitoa mfano wa aliyewahi kuwa Waziri Mkuu wa Malaysia, Dk. Mahathir Mohamed, aliyefukuzwa katika chama, lakini baadaye viongozi wa chama chao wakampigia magoti na kumuomba msamaha.
“Alivyorudi katika chama alipata nafasi ya kuwa waziri mkuu, nafasi aliyoitumikia kwa miaka 22,” alisema Zitto.

Alisema pia Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad, alifukuzwa CCM, lakini leo ni mmoja wa viongozi wa nchi hii.

“Kwa hiyo wazee wangu nawaombeni, kwa hatua yoyote nitakayochukua kuhusu mustakabali wa hatma yangu ya kisiasa mniunge mkono,” alisema Zitto.

Baada ya mkutano wa jana wa kuzungumza na wawakilishi hao kutoka vijiji 45 vya jimbo hilo, leo anatarajiwa kufanya ziara na pamoja na mambo mengine, atakagua utekelezaji wa ahadi zake alizotoa alivyoomba kura mwaka 2010.

Kesho anatarajiwa kufanya mkutano mkubwa wa hadhara katika makao makuu ya jimbo hilo, Mwandiga, ambapo anatarajiwa kutangaza mustakabali wake wa kisiasa.

Hivi karibuni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kilitangaza kumvua Zitto uanachama, hatua iliyofikiwa baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kutupa shauri lililofunguliwa na mbunge huyo akipinga kujadiliwa na Kamati Kuu ya chama hicho.

Hatua hiyo ilizua utata baada ya wakili wake, Albert Msando, kudai hawakuwa na taarifa ya uendeshwaji wa kesi hiyo hadi ilipotolewa uamuzi.

Katika hatua nyingine, Ofisi ya Bunge imenukuliwa na vyombo vya habari ikisema haijapata taarifa ya uamuzi huo na ikiipata itafanya uchunguzi ili kujiridhisha kama taratibu zilifuatwa hadi ukatolewa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles