26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Zitto aweka wazi mikakati ya uchaguzi

Na ANDREW MSECHU

KIONGOZI wa chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe, ameweka wazi mikakati ya chama hicho kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, huku akivitaka vyombo vya usalaa kuhakikisha vinatimiza wajibu wake wa kulinda raia dhidi ya matukio ya utekaji ambayo yamejitokeza hivi karibuni.

Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam jana, Zitto aliwatambulisha rasmi viongozi wa timu ya kampeni ya kitaifa ya chama hicho, akisemea wamepewa jukumu la kusimamia na kuzungumzia masula ya uchaguzi ndani ya chama hicho.

Akianika timu yake Zitto alisema Mwenyekiti wa Timu ya kampeni atakuwa, Joram Bashange ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Bara na Mjumbe wa Kamati Kuu huku Wakili Emmanuel Lazarus Mvula akiwa Meneja wa kampeni.

“Kwa hiyo kwa kuwa tayari kama mlivyoona, viongozi wote wa juu wa chama, yaani mimi ninakwenda jimboni kuwania ubunge, Mwenyekiti wa chama, Maalim Seifa anawania urais wa Zanzibar, Katibu Mkuu Ado Shaibu anakwenda kuwania ubunge jimboni, kwa hiyo hawa niliowataja ndio watakaokuwa na jukumu la kusimamia na kusemea chama.

“Kwahiyo katika kipindi chote hiki cha kampeni hadi uchaguzi, Bashange na Mvula ndio watakaosimamia shughuli zote za kampeni na kuratibu mienendo yote, pia watakisemea chama katika masuala ya kampeni, ndio watakaokuwa na taarifa zote zitakazohitajika,” alisema 

Katika mkutano huo, Zitto pia alizungumzia matukio ya utekwaji, kupigwa na kujeruhiwa kwa wanachama na wagombea wao waliotia nia katika nafasi ya ubunge na udiwani.

 Alidai wagombea wao waliofanyiwa vitendo hivyo ni wa Jimbo la Ruangwa mkoani Lindi huku akilitaka jeshi la polisi kuhakikisha linafanya upelelezi na kuwanasa waliohusika.

Aliwataja wahanga wa matukio hayo kuwa ni aliyeshika nafasi ya pili kwenye kura za maoni ndani ya chama hicho katika Jimbo la Ruangwa, Said Ally Nangendekwa ambaye alipigwa na kujeruhiwa akiwa nyumbani kwake Agosti 9, 2020.

Alisema mwingine ni Joakim Ng’ombo ambaye alitekwa, kupigwa Agosti 12 na kuokotwa wilayani Mkuranga mkoani Pwani Agosti 13 akiwa na hali mbaya ambapo awali alitibiwa katika Hospitali ya Temeke na sasa amehamishiwa Hosptali ya Taifa ya Muhimbili baada ya hali yake kuzidi kuwa mbaya zaidi.

Zitto alisema Ng’ombo ndiye aliyeteuliwa na ACT Wazalendo kuwania nafasi ya ubunge katika Jimbo la Ruangwa.

 “Kwa hiyo, kutokana na matukio haya, ninaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ifuatilie kwa karibu na kutolea ufafanuzi matukio haya kama ni ya kisiasa basi ikemee na kuchukua hatua.  Wanachama wa ACT Wazalendo wachukue hatua za kujilinda, kulinda viongozi wao na mali za chama.

“Pia chama kinawaagiza wanachama wote kufuata taratibu za kisheria wakati wote kuelekea Uchaguzi Mkuu na pale wanapoona haki zao au haki za wengine zinavunjwa watetee na kuzuia uvunjwaji wa haki kwa kuripoti matukio hayo mahali panapohusika,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles