27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Zidane ataweza kurudisha heshima ya Real Madrid?

BADI MCHOMOLO

MIONGONI mwa vitu ambavyo vimechangia kwa mabingwa wa kihistoria wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Real Madrid kushindwa kufanya vizuri msimu huu ni kutokana na kuondoka kwa kocha wao Zinedine Zidane.

Zidane aliondoka ikiwa ni siku chache baada ya kuipa timu hiyo ubingwa wa tatu mfululizo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kuwafunga Liverpool mabao 3-1, hivyo nafasi yake ikachukuliwa na Santiago Solari, ambaye alikuwa kocha wa timu ya Taifa ya Hispania kwa wakati huo.

Solari halishindwa kuwatumia wachezaji hao ambao waliandika historia ya kubeba taji hilo kubwa kwa misimu mitatu mfululizo, hakuna kikubwa ambacho alikiongeza, ila inaonekana kwamba halishindwa kuwatumia wachezaji hao.

Hiyo ilikuwa moja ya sababu, lakini sababu nyingine ni kuondoka kwa aliyekuwa mshambuliaji wao hatari Cristiano Ronaldo.

Ronaldo alikuwa mmoja kati ya wachezaji wenye mchango mkubwa wa mafanikio ya timu tangu alipojiunga mwaka 2009.

Baada ya kuisaidia Real Madrid kuchukua taji hilo la Ligi ya Mabingwa mwaka jana, mchezaji huyo aliondoka na kujiunga na klabu ya Juventus ambayo anaitumikia kwa sasa.

Kuondoka kwa wawili hao kukaacha pengo kubwa ambapo hadi sasa linaonekana kuwa wazi. Madrid wamejikuta wakiondolewa kwenye michuano hiyo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya katika hatua ya 16 bora dhidi ya Ajax ikiwa ni mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 22.

Hata hivyo, kwenye michuano ya Ligi Kuu Hispania timu hiyo inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi huku Atletico Madrid wakishika nafasi ya pili na nafasi ya kwanza ikiendelea kushikiriwa na mabingwa watetezi Barcelona.

SPOTIKIKI imekufanyia uchambuzi wa kina ambao Zidane anaamini anaweza kurudisha heshima ya timu hiyo kutokana na mambo sita.

Kupewa huru

Hii ni moja kati ya pointi ambayo Zidane aliomba kutoka kwa rais wa timu hiyo Florentina Perez. Wakati wanazungumza juu ya kumrudisha kuwa kocha mkuu kitu cha kwanza alichokiomba ni kupewa uhuru wa kufanya kazi yake.

Kumekuwa na madai kwamba, baadhi ya makocha wamekuwa wakiingiliwa kwenye majukumu yake ya kazi hasa pale anapofanya maamuzi ya kuwachukulia hatua wachezaji.

Hivyo Zidane anaamini akipewa uhuru wa kazi, atahakikisha anarudisha heshima ya timu hiyo ambayo ilianza kupotea tangu kuondoka kwake.

Kuuza wachezaji

Kocha huyo mpya anaamini katika kikosi cha timu hiyo kuna wachezaji ambao hawafai kuitumikia timu, hivyo akisema wachezaji hao wauzwe basi kitendo hicho kifanyike.

Hata kama hakitofanyika, basi akiamua kumuacha benchi kusitokee na mtu yeyote kumpigia kelele kwa nini mchezaji fulani anaachwa benchi.

Uwepo wa Marcelo na Isco

Hawa ni miongoni mwa wachezaji ambao wanatajwa kutakiwa kuondoka mara baada ya kumalizika kwa msimu huu.

Marcelo anahusishwa kutaka kumfuata rafiki ya Cristiano Ronaldo katika klabu ya Juventus, wiki kadhaa zilizopita beki huyo wa pembeni aliweka wazi kupitia ukurasa wake wa Twitter kwamba ana kila sababu ya kuondoka na anavutiwa kujiunga na Juventus.

Hata hivyo, inasemekana kuwa Ronaldo anachochea mchezaji huyo kutua katika klabu hiyo ya Bibi Kizee wa Turin.

Kwa upande mwingine Isco ni mmoja kati ya wachezaji ambao walikuwa na nafasi kubwa chini ya Zidane misimu iliopita, lakini baada ya kuondoka mchezaji huyo amekua akikosa nafasi ya kudumu katika kikosi cha kwanza chini ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo Solari.

Kutokana na hali hiyo Isco aliweka wazi kuwa, haoni sababu ya kuendelea kuwa mchezaji wa timu hiyo, hivyo ni wakati wa kuondoka huku Manchester City ikiwa chini ya kocha wake Pep Guardiola ikiwa na lengo la kuinasa saini ya mchezaji huyo mwishoni mwa msimu huu.

Lakini ujio wa Zidane ndani ya Madrid, unaweza kurudisha furaha za wachezaji hao kwa kuwa ameomba kuwazuia kuondoka kwao.

Neymar hasisajiliwe

Rais Perez amekuwa akisikika kua na nia ya kutaka kumsajili Neymar raia wa nchini Brazil ambaye kwa sasa anakipiga katika klabu ya PSG.

Neymar anahusishwa kutaka kurudi nchini Hispania ikiwa pamoja na klabu yake ya zamani ya Barcelona, lakini Zidane amedai kwamba hakuna sababu ya Madrid kumsajili mchezaji huyo.

James Rodriguez

Huyu ni nyota wa Real Madrid ambaye kwa sasa anakipiga katika klabu ya Bayern Munich kwa mkopo, kumekuwa na taarifa kwamba kutokana na kiwango anachokionesha mchezaji huyo Madrid wanataka kumrudisha.

Lakini Zidane amedai hayupo kwenye mipango yake, hivyo ni bora akaachwa aendelea kuitumikia Bayern Munich kwa mkopo au kuuzwa moja kwa moja.

Usajili wa Mbappe

Rais Perez alikuwa kwenye mipango ya kuboresha kikosi hicho kwa kuwasajili nyota wa PSG, Neymar na Kylian Mbappe mara baada ya kumalizika kwa msimu huu, lakini Zidane amedai Madrid wapambane kuhakikisha wanaipata saini ya Mbappe.

Kwa kufanya hivyo, kocha huyo amewahakikishia heshima ya Real Madrid itarudi kama ilivyo misimu iliopita.

Wapo ambao wameshangaa kuona Zidane akirudi Madrid, wanaamini maamuzi hayo yanaweza kuja kushusha heshima yake kutokana na kile alichokifanya akiwa na timu hiyo kwa miaka ya nyuma, bora angeacha historia aliyoiweka Madrid na kwenda kujiunga na klabu zingine.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles