24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Zamu ya Serengeti Boys hadi Kombe la Dunia

TIMU ya soka ya Taifa ya vijana walio chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’, kwa sasa ndiyo jicho pekee linalotazamwa na Watanzania kutokana na kuwa kwenye majukumu mazito ya kulipigania Taifa.

Serengeti Boys inayonolewa  na kocha mkuu, Oscar Milambo, kwa sasa ipo nchini Rwanda kushiriki mashindano  maalumu ya maandalizi ya Afrika (Afcon-17) kwa vijana wa umri huo yatakayofanyika nchini kuanzia Aprili 14 hadi 28, mwaka huu.

Mashindano haya ya Afcon-17 yana umuhimu mkubwa kwa Tanzania kwa kuwa iwapo timu hiyo ya Serengeti Boys itamaliza kwenye nafasi mbili za juu, itaweza kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Dunia kwa vijana wa umri huo zitakazofanyika nchini Brazil, Oktoba mwaka huu.

Katika mashindano hayo ambayo mechi zake zitachezwa kwenye Uwanja wa Taifa na Azam Complex, Dar es Salaam, Serengeti Boys imepangwa kundi A ikiwa na timu za Uganda, Angola na Nigeria, wakati kundi B lina timu za Cameroon, Senegal, Morocco na Guinea.

Hii ni fursa nyingine kwa Tanzania kujitangaza kwenye medani ya soka la kimataifa na kufungua milango ya wachezaji kucheza katika ligi mbalimbali barani Afrika na Ulaya kwa ujumla. 

Hii ni mara ya pili kwa Serengeti Boys kushiriki Afcon ya vijana walio chini ya miaka 17, itakumbukwa kuwa mara ya kwanza ilishiriki fainali hizo mwaka 2017 na kutolewa na Niger katika hatua ya makundi baada ya kufungwa bao 1-0.

Hii ni zamu ya Serengeti Boys kutoka Afcon hadi Kombe la Dunia, ni wazi kuwa kwa maandalizi waliyoyapata, wana nafasi ya kufuzu kwa Kombe la Dunia nchini Brazil.

Watanzania wana matumaini makubwa na Serengeti Boys kufanya vizuri kwenye michuano hiyo ya Afcon ya vijana na kukata tiketi ya Kombe la Dunia kutokana na maandalizi mazuri waliyoyafanya.

Pamoja na sasa kushiriki mashindano hayo maalumu ya maandalizi nchini Rwanda, lakini pia ilishiriki michuano ya ‘UEFA Assist’ iliyofanyika nchini Uturuki.  

Sisi MTANZANIA tuna imani na Serengeti Boys kama ilivyokuwa kwa Taifa Stars iliyofuzu Fainali za Afrika itakayofanyika nchini Misri kuanzia Juni mwaka huu.

Tunaamini kwamba, Serengeti Boys itafanya vizuri kwenye mashindano ya Afcon kwa vijana na kufuzu kwa Kombe la Dunia.

Kufuzu kwa Serengeti Boys kwenye Kombe la Dunia, kutaongeza chachu kwa Taifa Stars nayo kusaka tiketi ya kufuzu fainali hizo ambazo tangu zichezwe kwa mara ya kwanza mwaka 1930 nchini Uruguay, Tanzania haijawahi kushiriki.

Tunaamini kuwa Serengeti Boys itafungua milango pia kwa wachezaji wa Taifa Stars kupigania kufuzu kwa Kombe la Dunia, baada ya kufuzu Afcon mwaka huu, michunao itakayofanyika nchini Misri kwa mara ya pili baada ya kufuzu mwaka 1980 nchini Nigeria.

Imani ya Watanzania wote ni kuona wanapata faraja kupitia timu hizo zinazoshiriki kwenye michuano mikubwa na kuitangaza Tanzania kimataifa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles