24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Zaidi ya Sh milioni 170 zasaidia kutatua changamoto ya macho kwa wananchi Kwimba

Na Clara Matimo, Kwimba

Katika kila kundi la watu 100 basi 20 wanakuwa na matatizo ya macho kati yao, sita wanaupungufu wa kuona unaotibika kwa miwani lakini mmoja atakuwa ni mlemavu wa kutokuona kabisa.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel,(kulia) akizindua jengo la kliniki ya huduma za macho ijulikanayo kwa jina la Roshanali Nasser Eye  lililopo katika hospitali ya Ngudu Wilaya ya Kwimba leo lililojengwa kwa ufadhili wa Dk. Moes Nasser raia wa nchini Marekani kwa gharama ya Sh milioni 55, kushoto ni Meneja Mradi wa kliniki hiyo, Eden Mashayo. Picha na Clara Matimo.

Takwimu hizo zimetolewa leo Julai 29, 2021 wilayani Kwimba mkoani Mwanza na Meneja Mpango wa Taifa wa Huduma za Macho kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsi, Wazee na Watoto, Dk. Bernadetha Shilio, wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa  jengo la Kliniki ya kutolea huduma ya afya ya macho ijulikanayo kwa jina la Roshanali Nasser Eye lililopo katika hospitali ya Ngudu Wilaya ya Kwimba lililogharimu zaidi ya Sh milioni 170 huku akibainisha kwamba katika kila hao watu 20 zaidi ya asilimia 80  ya matatizo yao yanatibika kwa njia ya miwani au upasuaji.

“Wagonjwa hao wa macho matibabu yao ni rahisi kabisa kwani upasuaji unachukua takribani dakika 10 hadi 15 na mgonjwa anapona na kuona vizuri kabisa na kuendelea na shughuli za uzalishaji mali vilevile kati ya mtu mmoja ambaye haoni kabisa asilimia 50 inaletwa na tatizo la mtoto wa jicho,” amesema Dk. Shilio.

Ili kutatua changamoto hiyo kwa wananchi wa Wilaya ya Kwimba mdau wa afya ya macho ambaye ni mtaalamu wa upimaji wa miwani (Optometria), Dk. Moes Nasser, raia wa nchini Marekani amewezesha ujenzi wa jengo la kliniki lilioogharimu Sh milioni 55 na vifaa tiba vilivyogharimu Sh milioni 115, 404, 900 ambaye ameomba kliniki hiyo ipewe jina la baba yake mzazi Roshanali Nasser.

Akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza pamoja na wananchi wa Wilaya ya kwimba kwa njia ya mtandao kutoka nchini Marekani leo wakati wa hafla ya uzinduzi wa jengo hilo la kliniki, Dk Nasser amesema ameamua kujenga hatua hiyo imelenga  kuwasogezea karibu huduma za macho wananchi wa Kwimba ikiwa ni kurudisha fadhila kwa nchi  kwani amezaliwa wilayani humo.

“Nimezaliwa Kwimba hivyo nimeona kidogo nilichojaliwa na Mwenyezi Mungu sinabudi kugawana na Watanzania wenzangu maana na mimi najisikia fahari kuzaliwa kwenye nchi ya watu wenye upendo naomba huduma zinazotolewa ziwe endelevu.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel, akizindua jengo hilo la kliniki na huduma za macho ameuagiza uongozi wa wilaya ya Kwimba kuhakikisha vifaa tiba vinatunzwa na vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa huku akimtaka  Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk. Thomas Rutachunzibwa, ahakikishe kumbukumbu sahihi zinahifadhiwa huduma zinazotolewa na wanaohudumiwa wafahamike.

“Isije ikawa tunawatengenezea mwanya baadhi ya watumishi wachache wasio waaminifu ambapo kihistoria wamekuwepo watu wa aina hiyo mgonjwa anakuja kutibiwa anaambiwa njoo usiku anampa huduma halafu fedha anaweka mfukoni, tutafuatilia kwa kina kuhakikisha huduma inayotolewa hapa inawafikia walengwa maana tumekuwa tukivunja na kuuwa miradi sisi wenyewe.

“Kumbuka yuko mwananchi ambaye ni Dk. Moes Nasser, amejinyima fedha hizo angeweza kuzitumia na familia yake, lakini ameleta hapa ili wananchi wapate huduma karibu  huu ni mchango mkubwa wa kizalendo hivyo ni wajibu wetu kuonyesha uadilifu wa hali ya juu, jengo hili lilianza kujengwa mwaka 2013 Serikali tulikutana na changamoto lakini mfadhili huyu mzalendo ametushika mkono”amesema.

Mhandisi Gabriel amesema serikali inaendelea kuboresha huduma za afya ikiwemo macho kwa kujenga  majengo,  sehemu ya kutolea huduma,  wataalamu, vifaa tiba na mahitaji mengine ya kutolea huduma  lengo ni kuwapa huduma wananchi wake ili wawe na afya bora inayowawezesha kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo waweze kuinua uchumi wa taifa.

Mmoja wa wagonjwa ambao wamepata fursa ya kuzindua kliniki hiyo kwa  kufanyiwa upasuaji wa macho aliyekuwa anasumbuliwa na mtoto wa jicho,  Revocatus Magesa (68)  amesema uwepo wa kliniki hiyo wilayani  humo umemrahisishia kupunguza gharama ambazo ingemlazimu asafiri hadi Mkoani Mwanza katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekoutoure au ya kanda, bugando kufuata matibabu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles