23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga watuma salamu Singida United

Theresia Gasper-Dar es salaam

KIKOSI cha Yanga SC, jana kilianza safari kuelekea Singida kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Singida United unaotarajiwa kuchezwa kesho Uwanja wa Namfua.

Yanga wanaenda Singida wakiwa wametoka kupoteza mechi mbili mfululizo ikiwa dhidi ya Kagera Sugar kwa kufungwa mabao 3-0 huku mchezo wa pili ukiwa dhidi ya Azam FC ambapo Yanga ilikubali kichapo cha bao 1-0, kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Kikosi hicho kiliondoka na wachezaji 20 kwenda kwa ajili ya mchezo huo ambao wamepania kuanza kuwapa furaha wapenzi na mashabiki wao baada ya kuwaacha na uzuni kwenye michezo miwili iliyopita.

Yanga itakutana na Singida United ikiwa na kumbukumbu ya kupata ushindi wa mabao 2-0 katika mchezo wa mzunguko wa kwanza kwenye dimba la Taifa.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa klabu hiyo, Hassan Bumbuli, alisema wachezaji wote waliopo safarini wapo vizuri na kila mmoja ana morali ya juu kwa ajili ya kurudisha furaha kwa mashabiki zao.

“Tunafahamu tumepata matokeo yasiyoridhisha huko nyuma na sasa tunaenda kwenye mchezo wetu mwingine dhidi ya Singida United, tumepanga kupamabana na kupata pointi tatu muhimu,” alisema Bumbuli.

Alisema wanafurahi kuona mashabiki wao wanaendelea kuwapa sapoti licha ya kukosa matokeo mazuri kwenye michezo miwili mfululizo.

Mashabiki wa klabu hiyo wameanza kuwasema vibaya wachezaji wao baada ya michezo hiyo miwili, hivyo Bumbuli aliongeza kwa kusema, kila mchezaji amesema yupo tayari kuipigania timu kwa michezo yote iliyopo mbele yao.

Katika msimamo wa Ligi, Yanga SC wanashika nafasi ya saba wakijikusanyia pointi 25 baada ya kucheza michezo 14, wakiwa sawa na Lipuli FC wanaoshika nafasi ya sita lakini wanatofautiana kwa idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Yanga watahakikisha wanashinda mchezo huo ili kuendana na kasi ya wapinzani wao Simba SC ambao wamekuwa wakipata matokeo mazuri kwenye michezo yao na kuwafanya kuwa vinara wa Ligi Kuu kwa pointi 41, wakifuatiwa na Azam FC wenye pointi 32.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles