24.4 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga watua salama Uturuki

yanga*Yapata safu mpya wajumbe Kamati ya Utendaji

*Wadhamini waipongeza, wakabidhi kitita cha ubingwa

NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

MABINGWA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga wametua salama nchini Uturuki walipokwenda kwa ajili ya kuweka kambi ya muda mfupi kabla ya kuivaa Mo Bejaia ya Algeria katika mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi Kombe la Shirikisho barani Afrika.

Katika kuhakikisha wachezaji wapo fiti kwa maandalizi ya mchezo huo utakaopigwa Juni 19, mwaka huu katika Uwanja wa Unite Maghrebine, uliopo mjini Bejaia, wachezaji wa Yanga wamefikia katika hoteli ya kifahari yenye mandhari ya kuvutia.

Kikosi cha Wanajangwani hao kiliondoka nchini jana alfajiri kuelekea nchini humo, huku beki mahiri wa kutegemewa, Juma Abdul, akiachwa kutokana na kusumbuliwa na majeruhi.

Lakini kocha Hans van der Pluijm alimuunganisha katika kikosi hicho beki mpya, Hassan Ramadhani ‘Kessy’ ambaye alisajiliwa akitokea kwa mahasimu wao, Simba na anatajwa kuziba pengo la Abdul Yanga itakapovaana na Mo Bejaia.

Kikosi cha Yanga kiliondoka baada ya kumalizika kwa zoezi la uchaguzi mkuu wa klabu hiyo ambao Pluijm naye alipata fursa ya kupiga kura kuchagua viongozi anaowataka.

Uchaguzi huo uliofanyika kwa utulivu wa hali ya juu, uliwaingiza madarakani viongozi 10 watakaoongoza kwa miaka minne ijayo ambao ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wanane wa Kamati ya Utendaji.

Katika uchaguzi huo uliofanyika Jumamosi iliyopita na matokeo yake kutangazwa jana ilishuhudia sura nane mpya hususani katika ujumbe wa kamati ya utendaji ambao ni Siza Lyimo (1,027), Omary  Amir (1,069), Thobias Lingalangala (889), Salim Nkemi (818),  Hashim Abdallah (727), Ayoub Nyenzi (889), Samuel Lukumay (818) na Hussein Nyika (770).

Wagombea walioshindwa kwenye kinyang’anyiro cha ujumbe na idadi ya kura walizopata kwenye mabano ni  David Luhago (582), Godfrey Mheluka (430), Ramadhani Kampira (182), Edgar Chibura (72), Mchafu Chakoma (69), George Manyama (249), Bkari Malima (577), Lameck Nyambaya (655), Beda Tindwa (452), Athuman Kihamia (558), Pascal Lizer (178) na Silvester Haule (197).

Wakati huo huo, wadhamini wa timu hiyo Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia ya Kilimanjaro, jana walikabidhi hundi ya Sh milioni 25 kwa klabu hiyo baada ya kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu wa 2015/16.

Akizungumza katika hafla fupi ya kuipongeza Yanga iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, Pamela Kikuli, alisema wao kama wadhamini wamefarijika kwa mafanikio ya klabu hiyo kutetea taji hilo kwa msimu wa pili mfululizo.

“Hii imedhihirisha wazi kuwa Yanga ni timu bora kwa msimu wa pili mfululizo ambapo ni mara ya sita tangu tuanze kuidhamini timu hiyo, hivyo ni faraja kwetu kwa sababu tunajivunia kuwekeza sehemu iliyo na mafanikio ya ushindi,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles