23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Wizara ya Elimu yaipatia NIT Bilioni 49 kuanzisha kituo cha umahiri

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa EASTRIP imekipatia Chuo cha Usafirishaji (NIT) zaidi ya Sh bilioni 49 kwa ajili ya kukiwezesha Chuo hicho kuanzisha Kituo cha Umahiri cha Mafunzo ya Taaluma ya Usafiri wa Anga na Operesheni za Usafirishaji.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu, Prof. Carolyne Nombo wakati akizindua vifaa vya mafunzo ya uhandisi na matengenezo ya ndege vilivyonunuliwa na mradi huo.

Amesema fedha hizo ni mkopo kutoka Benki ya Dunia zimetolewa kwa chuo hicho kwa kutambua mchango wake katika kuandaa wataalamu wenye weledi na ujuzi katika fani za usafirishaji na uchukuzi.

Prof. Nombo amesema Serikali ya Awamu ya Sita imekuwa ikifanya kila linalowezekana ili kuhakikisha mafunzo yanayotolewa katika vyuo vyetu yanaakisi mahitaji ya sekta husika na hivyo kupata wahitimu wenye kuendana na mahitaji ya soko la ajira.

Akizungumzia vifaa maalum vilivyozinduliwa kwa ajili ya uhandisi wa matengenezo ya ndege amesema Serikali imetumia kiasi cha Sh bilioni 2.1 kwa ajili ya kukiongezea chuo uwezo wa kutoa elimu bora kwenye taaluma ya uhandisi wa matengenezo ya ndege.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha vyuo vya kimkakati kama hiki cha NIT, DIT na ATC vinatoa mafunzo yanayoakisi maendeleo ya nchi na yanayolenga kutatua changamoto zinazowakabili wananchi,” amesema Prof. Nombo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji, Mhandisi Prof. Blasius Nyichomba ameishukuru Serikali kwa kukiwezesha chuo hicho kupata vifaa vya kisasa vitakavyowezesha utoaji wa elimu katika Chuo hicho.

Naye Mkuu wa Chuo Mhandisi Prof. Zacharia Mganilwa ameeleza kuwa vifaa vilivyonunuliwa ni “runnable jet engine, motorized cutaway piston engine na virtual maintainance trainer” ikiwa ni moja ya mafaniko ya utekelezaji wa mradi huo.

Mmoja wa wanafunzi wa fani ya uhandisi matengenezo ya ndege wa chuo hicho, Makame Abdalla ambae amebuni mfumo wa uondoshaji barafu kwenye mabawa ya ndege ameishukuru Serikali kwa kukiwezesha chuo hicho kupata vifaa vya kujifunzia na ametoa rai kwa wanafunzi wanaotaka kusoma fani hiyo kusoma NIT kwa kuwa kina vifaa vya kutosha katika fani hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles