BEATRICE KAIZA Na KYALAA SEHEYE-DAR ES SALAAM
BAADA ya siku 21 za kutoka mahabusu, wasanii mbalimbali waliokamatwa katika awamu ya kwanza ya orodha ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akiwatuhumu kujihusisha na dawa za kulevya, wamefunguka na kuelezea mambo waliyopitia wakiwa mahabusu kabla ya kupatiwa dhamana mahakamani.
Wema Sepetu
Akizungumza na MTANZANIA kwa simu jana, msanii maarufu wa filamu nchini, Wema Sepetu, alisema hana cha kuzungumza kwa sababu bado ana kesi mahakamani.
“Kwa kifupi mahabusu siyo kuzuri. Sina cha kuzungumza kwa kuwa bado nina kesi mahakamani,” alisema na kuongeza:
“Hakuna asiyejua kama mahabusu si sehemu nzuri ila nashukuru Watanzania wananipenda kuliko ninavyofikiria kwa sababu nimepeta marafiki wengi na kila mmoja alikuwa akitaka kuongea na mimi, nitaongea vizuri kesi itakapokwisha,” alisema Wema.
TID
Msanii wa muziki wa bongo fleva, Khalid Mohamed a.k.a TID aliweka wazi kukaa mahabusu kwa wiki nzima kuwa ndicho kitu kilichomuathiri zaidi.
Alisema hiyo ni kwa sababu kule kuna watu mbalimbali wakiwamo wahalifu wa aina tofauti ambao walimbugudhi kwa vile yeye ni maarufu na kwamba kimsingi jambo hilo lilimkwaza sana.
Hata hivyo, alimshukuru Makonda kwa kampeni yake ya kupambana na dawa za kulevya kwamba imefungua ukurasa mpya kwake.
“Kwa upande wangu vita hii imebadilisha mfumo wa maisha yangu, TID wa miaka mitano nyuma si TID wa sasa. Naamini ambaye anafuatilia kazi zangu kwa umakini na nina uhakika nitasonga mbele. Bila kampeni ya Makonda hadi sasa sijui ningekuwa wapi,”alisema.
TID alifafanua kuwa mara nyingi alikuwa akikana kutumia dawa za kulevya lakini baada ya kukiri na kusaidiwa wiki tatu zilizopita anaona mafanikio makubwa mbele yake.
Aliwataka mashabiki wake kukaa mkao wa kula kwa sababu sasa ameamua kufuatilia kazi zake alizokwisha kuziandaa lakini alishindwa kwa sababu ya ‘uteja’
Ahmed Hashim ‘Petitman’
Meneja wa msanii, Bill Nas na Cantury Boy alidai kuwa kitendo cha kuwekwa mahabusu kimempotezea mipango mingi ambayo imekjwama kwa muda.
“Hili suala linaniuma sana na ndiyo maana sipendi kulizingumzia sababu limenipotezea msingi wangu. Wasanii wangu ambao nawasimamia ila namshukuru Mungu niko huru naendelea na mambo yangu,” alisema Petitman.
Akielezea maisha ya mahabusu, msanii huyo alisema amejifunza vitu vingi na kukutana na watu wengi ingawa alikuwa akikosa raha kukaa mbali na familia yake.
TID aliwashauri vijana kuachana na biashara haramu na kufanya vitu ambavyo vitawaletea matatizo na kwamba kupitia kwao wapate fundisho.
“Mimi na Wema ni familia kwa sababu ni watu tulioishi kwa muda mrefu, tunaheshimiana… niliondoka Endless Fame niweze kufungua kampuni yangu kutafuta maisha yangu na sasa namiliki kampuni inayoitwa living fast living good ‘LFG’.
Tunda
Msanii wa kupamba video, Anna Kimario maarufu Tunda, aliweka wazi kuwa kitendo cha kukaa mahabusu kimemvunjia hadhi na heshima ya kuaminika mbele ya jamii.
Alisema kukamatwa kwake kumesababisha watu waliotarajia kumpa mkataba wa kwenda kurekodi video kukatisha mawasiliano jambo ambalo alisema ni kero na fedheha kwake.
“Kukaa mahabusu si sehemu salama, imenifanya nimekumbana na matatizo mengi kwenye familia yangu ambayo ilikuwa ikiniamini.
“Pia imenipotezea mkataba wangu wa kufanya kazi nje ya nchi niliokuwa naamini sasa naanza kujulikana kimataifa,” anasema Tunda.