30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Waziri Ummy azindua mashine za bil 13/- kuchunguza damu

Na CLARA MATIMO- MWANZA

WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsi, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu  amezindua mashine nne  kati ya 24 za kupima maambukizi ya magonjwa mbalimbali katika damu na makundi ya damu zenye thamani ya Sh bilioni 13.

Alifanya uzinduzi huo jijini hapa juzi, wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wachangia Damu Duniani yaliyofanyika kitaifa  mkoani  hapa.

Ummy alisema mashine mbili zitatumika kupima magonjwa makuu manne ambayo mchangia damu anapaswa kupima ili damu yake  iweze kutumiwa na wahitaji.

Alisema magonjwa hayo, ni virusi vya Ukimwi (VVU), kaswende, virusi vya homa ya ini B na C na mbili zinapima makundi ya damu.

“Nimefurahi kuzindua mashine mpya nne za kisasa ambazo tumezifunga, zitasaidia kuondoa changamoto zilizokuwa zikiukabili Mpango wa Taifa wa Damu Salama, maana zilizotumika awali zilichukua muda mrefu kupima sampuli za damu.

“Tunataka kumfikia kila Mtanzania mwenye mahitaji ya damu salama popote alipo bila kikwazo chochote, nawasisitiza watoa huduma za afya wote nchini kutopokea hata senti tano kumpatia mgonjwa damu salama, ila naendelea  kuwaomba ndugu wachangie damu wanapokuwa na mgonjwa anayehitaji kuongezewa damu, tunaita ‘blood replacement’,” alisema.

Alisema  damu haiuzwi na Serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali kuhakikisha inapatikana katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Ummy alisema pia Shirika la Afya Duniani (WHO) limependekeza kila nchi ikusanye chupa za damu sawa na asilimia moja ya idadi ya wananchi wote au chupa 10 kwa kila watu 1,000 ili kukidhi mahitaji ya damu salama.  

“Inakadiriwa mwaka 2018 Tanzania ilikuwa na watu milioni 52.6, tunatakiwa kukusanya chupa 526,000 kwa mwaka,  tumeongeza  ukusanyaji  wa chupa 307,835 mwaka 2018, ikilinganishwa na chupa 233,953 mwaka 2017, ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 32.

“Bado hatujafikia pendekezo la WHO, makusanyo ya mwaka jana ni sawa na chupa sita kwa kila wananchi 1,000 ambayo ni asilimia 60 ya mahitaji ya nchi,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles