24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Waziri Ndaki apiga tafu maendeleo ya elimu Maswa

Na Samwel Mwanga, Maswa

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amechangia vifaa vya ujenzi kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari Mwang’honoli na nyumba tatu za walimu katika shule ya msingi Jihu wilaya ya Maswa mkoani Simiyu.

ashimba ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Maswa Magharibi wilayani humo amekabidhi vifaa hivyo katika mikutano ya hadhara iliyofanyika jana kwa nyakati tofauti tofauti katika kijiji cha Mwang’honoli na kijiji cha Jihu.

Katika mkutano wake wa awali katika kijiji cha Mwang’honoli ambapo alikabidhi vifaa vyenye thamani ya Sh 2,450,000 ambavyo ni mabati, mbao, misumari na mifuko 60 ya saruji amesema kuwa lengo ni kuhakikisha shule hiyo inakamilika kwa wakati Januari mosi mwakani ili iweze kusajiliwa na kufunguliwa ili wanafunzi wa kidato cha kwanza wanaanza masomo.

Amesema kuwa kukamilika kwa shule hiyo kutasaidia kupunguza umbali kwa wanafunzi wa Kata hiyo ambao wanasafiri umbali mrefu kwenda kusoma katika shule za kata jirani.

“Wanafunzi wenu wanasafiri umbali mrefu kutoka katika kata yenu ya Mwang’honoli hasa wanaochaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari ila tukikamilisha ujenzi wa shule hii kwa wakati hili tatizo litaondoka maana watasomea hapa hapa,”amesema.

Amesema kuwa ila amesikitishwa na kitendo cha uongozi wa Kata hiyo kushindwa kusimamia kikamilifu ujenzi wa shule hiyo wakati vifaa vyote vya ujenzi vipo na hivyo kumwagiza Mkuu wa wilaya hiyo, Aswege Kaminyoge kuhakikisha kuwa inakamilika ifikapo Januari mosi mwakani.

Katika mkutano wake wa hadhara katika kijiji cha Jihu aliwapongeza wananchi wa kijiji hicho kwa uamuzi wao wa kuamua kujenga nyumba tatu za walimu ili kupunguza tatizo la upungufu wa nyumba za kudumu za walimu katika shule hiyo.

Amesema katika kuunga juhudi zao ameamua kuchangia vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya Sh 2,242,000 ambavyo ni mabati, mbao, misumari  pia alijitolea kulipa gharama za fundi ambaye ataezeka nyumba hizo.

“Nimefurahishwa kwa kitendo chenu cha kuamua kujitolea kujenga nyumba hizo tatu za walimu huu ndiyo uongozi wa unaotakiwa wa kusaidiana katika shughuli za maendeleo nami nikiwa mbunge wenu ninawaunga mkono kwa kutoa vifaa hivi vya ujenzi,”amesema Ndaki.

Mkuu wa wilaya ya Maswa, Aswege Kaminyoge amemhakikishia Waziri Ndaki kuwa atasimamia kwa kikamilifu ili kuhakikisha miradi yote ya elimu hasa miundo mbinu ya madarasa na nyumba za walimu inakamilika kwa wakati.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles