Na Gurian Adolf-Sumbawanga
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, amewataka wananchi kuachana na mawazo kuwa ipo siku Serikali itakata eneo la hifadhi na kuwapatia kwa ajili ya shughuli zao.
Aliyasema jana wakati akizungumza na wananchi wa vijiji vya Lyazumbi na Kizi wilayani Nkasi mkoani Rukwa,baada ya wananchi kumuomba awamegee sehemu ya ardhi iliyopo Hifadhi ya Lwafi kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kiuchumi..
Alisema Tanzania bado ina sehemu kubwa ya watu kuendelea kufanyia shughuli zao, bali kilichokosekana ni kutokuwapo mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Alitoa kauli hiyo,baada ya mmoja wa wananchi katika Kijichi cha Lyazumbi, Hamisi Kiswaga kumuomba awamegee sehemu ya ardhi ndani ya hifadhi ili akipatie kijiji kwa lengo la kukipanua na kupata maeneo ya shughuli za kilimo.
Kutokana na hatua hiyo,Waziri Maghembe ameuagiza uongozi wa Wilayaya Nkasi kuhakikisha wanatengeneza kisima cha maji haraka katika Kijiji cha Lyazumbi ili wakazi wake waweze kupata maji ya kutosha.
Alisema hivi sasa wakazi wa kijiji hicho, wanategemea maji kutoka ndani ya hifadhi,baada ya bomba lao kuharibika na kuwa kitu hicho hakikubaliki.
“Ni kosa kubwa watu kutegemea huduma ndani ya hifadhi maana wanaweza kukumbana na majanga mbalimbali ndani ya hifadhi,sheria hairuhusu jambo hilo wilaya tengenezeni kisima hicho haraka ili kusiwapo mwingiliano kati ya hifadhi na mahitaji ya watu”alisema Maghembe