27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Waziri Kenya kuwania uenyekiti AU

Waziri ameiongoza Kenya kuandaa mikutano mbalimbali ya kimataifa ukiwamo wa biashara uliohutubiwa na Rais Barack Obama wa Marekani.. Aidha wizara yake imesimamia ziara za viongozi wa dunia akiwamo Rais Obama, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, Papa Francis na wengineo.

NAIROBI, KENYA

SERIKALI ya Kenya imewasilisha jina la Waziri wake wa Mambo ya Nje, Amina Mohamed kuwania uenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU).

Mwanadiplomasia huyo namba moja wa Kenya atakabiliana na Agapito Mba Mokuy wa Guinea ya Ikweta, Abdoulaye Bathily wa Senegal na Pelonomi Venson-Moitoi wa Botswana.

Ni Rais Uhuru Kenyatta aliyefichua suala hilo wakati  akihutubia mkutano wa kilele wa vijana Ikulu mjini hapa jana.

“Naona Amina anafanya kazi vyema. Tumemteua awanie uenyekiti wa AU,” Rais Kenyatta alisema.

Mbali ya uzoefu wake wa kidiplomasia, Mohamed anao uwezekano wa kushinda kwa vile hakuna taifa la Afrika Mashariki lililowahi kushika wadhifa huo.

Uchaguzi wa wajumbe wa Tume ya AU uliofanyika mjini Kigali, Rwanda Julai 2016 ulisitishwa baada ya raundi saba za upigaji kura kushindwa kutoa mgombea aliyepata theluthi mbili ya kura zinazohitajika kuchagua mwenyekiti.

Nafasi hiyo iko wazi baada ya kumalizika kwa muhula wa Nkosazana Dlamini-Zuma, ambaye amekuwa akiishikilia tangu mwaka 2012 na ambaye hakuomba kuwania muhula wa pili.

Hata hivyo, Zuma anaendelea na wadhifa huo hadi mwenyekiti mpya atakapopatikana katika kikao kijacho cha Januari 2017.

Jopo la uteuzi kufikia Oktoba 14 litasambaza oriodha ya wagombea walio tayari kwa uchaguzi huo.

Mohamed amekuwa katika utumishi wa umma kwa miaka 29 na aliwahi kuwa balozi wa Kenya na mwakilishi wa kudumu katika Umoja wa Mataifa (UN) mjini Geneva.

Katibu Mkuu wa UN Ban Ki-moon baadaye alimteua kuwa Msaidizi wa Katibu Mkuu na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la UN la Programu za Mazingira (Unep) mjini Nairobi.

Waziri ameiongoza Kenya kuandaa mikutano mbalimbali ya kimataifa ukiwamo wa biashara uliohutubiwa na Rais Barack Obama wa Marekani..

Aidha wizara yake imesimamia ziara za viongozi wa dunia akiwamo Rais Obama, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, Papa Francis na wengineo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles