Na Abubakari Akida, MOHA
Madereva wa bodaboda visiwani Zanzibar, wametakiwa kufuata sheria za usalama barabarani ili kuepusha ajali na vifo vilivyoshamiri ambavyo chanzo chake ni kukiuka sheria.
Rai hiyo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambae pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Khamis Hamza Chilo wakati wa kikao na madereva bodaboda wa Mkoa wa Mjini Magaharibi ambacho kilihudhuriwa na uongozi wa Jeshi la Polisi Mkoa.
“Serikali yenu sikivu chini ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi iko katika mchakato ili mruhusiwe kutoa huduma za usafiri katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar.
“Nawaomba muanze kujifunza na kufuata sheria za usalama barabarani ili tunayoona yanayotokea kule Bara yasitokee huku,” amesema Chilo.
Akizungumzia takwimu za ajali za bodaboda, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Kamishna Msaidizi wa Polisi Awadh Juma Haji,amesema ajali na vifo vimepungua kutokana na elimu inayotolewa kwa madereva hao wa pikipiki lengo ni kuhakikisha utii wa sheria bila shuruti unafuatwa.
“Mwaka huu tuna ajali 17, watu waliofariki mwaka jana ni watu 18 na mwaka huu tuna vifo 17 huku upungufu ukiwa ni mtu mmoja, lakini ajali zilizosababisha majeruhi kwa mwaka jana ni ajali 19 na mwaka huu ni ajali 6 kwa hiyo kuna upungufu wa ajali 15, watu waliojeruhiwa mwaka jana watu 37 na mwaka huu ni watu sita, tunaona kuna kushuka kwa ajali na athari zake” amesema RPC Awadh.
Wakizungumza kwa nyakati mbalimbali katika kikao hicho bodaboda hao waliiomba Serikali kuandaa utaratibu ili kuruhusiwa kufanya kazi zao visiwani hapo huku wakiahidi kuendelea kufuata sheria za usalama barabarani.