31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Waziri aagiza ukaguzi vituo vya kupoza umeme

Na Zuena Msuya-MBEYA

MAMENEJA wote wanaosimamia vituo vya kupoza na kusambaza umeme nchini wametakiwa kufanya ukaguzi wa kila siku asubuhi katika mitambo na mashine zilizopo katika vituo hivyo kuondoa adha ya kukatika umeme kutokana na hitilafu au uharibifu katika vituo hivyo, licha ya kuwa vituo hivyo vinafanyiwa ukarabati na ukaguzi wa kila mara au hata baada ya miezi kulingana na utaratibu waliojiwekea.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nishati, Dk. Medard  Kalemani, wakati wa ziara yake ya kikazi katika Jiji la Mbeya, baada ya kutembelea kituo cha  kupoza na kusambaza umeme kilichopo Mwakibete na kukagua miradi  ya kusambaza umeme katika Kijiji cha Nsalaga na Iduda inayotekelezwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Alisema kumekuwa na changamoto ya kukatika umeme kwa muda mchache katika baadhi ya maeneo na sababu kuu ya ikielezwa kuwa ni hitilafu katika vituo au kuharibika kwa kifaa katika kituo cha kupoza na kusambaza umeme.

Alifafanua kuwa changamoto hiyo inaepukika na kutoweka kabisa endapo wahandisi na mafundi watakuwa na tabia ya kufanya uchunguzi wa mitambo na mashine zao kila siku asubuhi kubaini tatizo kabla ya kutokea.

“Mafundi na wahandisi muwe na tabia ya kufanya ukaguzi na matengenezo ya kila siku asubuhi badala ya kusubiri tatizo litokee, achene kufanya kufanya ukaguzi na matengenezo kwa mazoea, hii itasaidia kufahamu mapema tatizo linazoweza kutokea baadaye na kuondoa usumbufu wa kukatika umeme kwa wananchi hali ya kuwa kuna umeme mwingi nawa kutosha,” alisema Kalemani.

Alisema serikali haitaki kuona mwananchi wake anaingia gharama ya kutumia jenereta kwakuwa nchi inazalisha umeme mwingi, pia inataka kuondokana na matumizi ya majenereta kwa kuimarisha njia ya usafirishaji, usambazaji pamoja na uzalishaji wa umeme nchini

“Mpango wa serikali ni kuachana na matumizi ya magenereta kwa watu wote, wakiwemo  wafanyabiashara, makampuni, mashirika na pia kuwapunguza gharama za maisha na kurahisisha utendaji wa kazi kuwa na umeme mwingi, wakutosha na ziada,” alisema  Kalemani.

Hata hivyo alisema kuwa ni lazima katika kila kituo cha kupooza na kusambaza umeme kiwe na stoo ya kuhifadhi vifaa vya dharura vitakavyotumika endapo ikatokea kifaa kimeharibika au kupata hitilafu.

Alisisitiza stoo hizo ni lazima ziwe na vifaa vizima na vya kutosha wakati wote, badala ya vifaa hivyo kuhifadhiwa katika ofisi za mameneja wa kanda au mikoa, hivyo kuleta usumbufu pindi tatizo linapotokea.

Akizungumzia huduma ya umeme wa viwandani, Dk. Kalemani alisema kuwa, viwanda vikubwa vipewe umeme wa peke yao wa kutosha na uhakika ili wazalishe kwa wingi waweze kulipa kodi na kuiingizia nchi mapato.

Alisema kwa kufanya hivyo kutaweza kuwabana wenye viwanda wanaokwepa kulipa kodi kwa kisingizo cha kutozalisha kutokana na kukosa huduma ya umeme.

Hivyo ametoa siku 10 kwa Tanesco, kufunga huduma ya umeme wa peke yake kwenye kiwanda cha kuzalisha Saruji Kiwanda cha Mbeya, ili kiweze kuajiri watu na wengi zaidi kuzalisha kwa wingi na kulipa kodi za serikali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles