24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Wazazi watakaozuia watoto kwenda Sekondari kukiona

Na Allan Vicent, Tabora

Wazazi na walezi wa watoto waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka huu wilayani Uyui Mkoani Tabora wametakiwa kuhakikisha watoto wao wanajiunga na shule hizo ili kutimiza ndoto zao la sivyo watawajibika.

Onyo hilo limetolewa juzi na madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo walipokuwa wakiongea na Mwandishi wa gazeti hili kwa nyakati tofauti wilayani humo.

Walisema kuwa moja ya majukumu ya diwani ni kuhakikisha watoto wote wa kike na kiume wanapata elimu kwa kuwa ni haki yao ya msingi, kinyume na hapo ni kukiuka taratibu, sheria na mwongozo wa serikali.

Diwani wa kata ya Ibiri, Yahya Mgeleka alisema mzazi au mlezi yeyote atakayeshindwa kupeleka mtoto wake sekondari ifikapo Januari 11 mwaka huu pasipo taarifa yoyote atakamatwa na kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Diwani wa kata ya Isila, tarafa ya Ilolangulu katika halmashauri ya wilaya ya Uyui Mkoani Tabora ambaye pia ni Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo, Said Ntahondi (mwenye kipaza sauti) akifungua kikao cha kwanza cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo hivi karibuni. Picha na Allan Vicent

Alibainisha kuwa wanataka watoto wote 266 waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka huu katika wilaya hiyo wawe wameanza masomo yao ifikapo Januari 11 mwaka huu bila kukosa na kama mzazi atapeleka mtoto wake shule binafsi hiyo haikatazwi ila atoe taarifa.

‘Mzazi au mlezi yeyote mwenye nia ya kuzuia mtoto wake kujiunga na shule ya sekondari kwa sababu yoyote ile ikiwemo kutaka kumwozesha atakumbana na mkono wa sheria, tunataka kila mtoto atimize ndoto zake kimaisha’, alisema.

Diwani wa kata ya Isila ambaye pia ni Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo hiyo, Said Ntahondi aliwataka Watendaji wa vijiji na kata kuanza kuwasiliana na Wakuu wa shule baada ya tarehe hiyo ili kupata takwimu za watoto walioripoti na ambao hawajaripoti kwa ajili ya hatua zaidi.

Alipongeza wadau mbalimbali wakiwemo wazazi na walezi kwa moyo wao wa kizalendo wa kuendelea kujitoa kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule zao watoto wote waliochaguliwa wapate nafasi.

 Alionya kuwa mzazi au mlezi yeyote atakayebainika kupanga njama za kuozesha mwanafunzi au mtoto wa kike aliye na umri wa chini ya miaka 18 atakamatwa na kufikishwa mahakamani mara moja.

Ntahondi alisisitiza kuwa hawataki kusikia habari yoyote kuhusu kuzuiwa mtoto kwenda shule, kuozeshwa au kutumikishwa katika shughuli za ufugaji au kilimo cha tumbaku ni marufuku , watoto wote ni lazima wasome.

Alisisitiza kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa, Dk. John Magufuli imelipa kipaumbele kikubwa suala la elimu ndio maana iliondoa ada na michango ya aina yoyote ili watoto wote wasome.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles