26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Wazazi Kagera watakiwa kuthamini elimu badala ya mijuburo

Na Nyemo Malecela, Kagera

Wazazi mkoani Kagera wametakiwa kuacha tabia ya kuchangia fedha nyingi katika mijuburo (kitchen part) na badala yake watumie fedha hizo kuwasaidia watoto wanaoshindwa kwenda shule kutokana na kukosa ada na mahitaji mengine ya shule.

Kauli hiyo imetolewa na Sheikhe wa Mkoa wa Kagera, Haruna Kichwabuta ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya kidato cha sita ya shule za Kaizilege na Kemebos zilizopo katika Manispaa ya Bukoba mkoani humo.

“Ninawaomba wakazi wa Mkoa wa Kagera wasiwe na hudhuru kwenye suala la kuwasomesha watoto, kwa sababu wazazi wengi wametawaliwa na kampeni za kuzigharamia sana ndoa badala ya kuwasaidia watoto wenye uhitaji wa mahitaji ya kusomea.

“Kwenye jamii kuna watoto wengi waokosa ada au kupungukiwa mahitaji ya kwenda shule hatumpeleki shule au kuchangia kama tunavyofanya kwenye mijuburo na badala yake tunasubiri kumpongeza kwenye mjuburo akisema amepata mchumba,” alisema Shekhe Kichwabuta.

Ameongeza kuwa: “Mimi nawashauri tuweke mijuburo ya kuchangia ada za watoto ili waweze kwenda shuleni ili ata wakiolewa au kuoa ile siku ya harusi anajua tayari ana shahada yake hawezi kulia kwenye harusi.

“Mara nyingi tumekuwa tukiwaona mabinti wetu wanalia kwenye harusi na sisi tunaongeza sauti na kuendelea kuimba eti ‘akanana kaile kona’ tukifikiri kuwa mtoto wetu analia kwa furaha kwa sababu ameolewa, kumbe tunashindwa kujua kuwa analia kwa sababu anafikilia hana elimu na hatukumuandalia mazingira yoyote ya kumuingizia kipato akiwa kwenye ndoa yake kwa sababu hatukumuchangia alipokosa ada na badala yake tumemchangia kufanikisha ndoa yake, wakati mwingine analia kwa sababu anakuwa na hasira na sisi ambao tumehudhu,” amesema Sheikh Kichwabuta.

Sheikhe Kichwabuta alisema mtu ambaye hakupata elimu ni mfu ambaye anatembea duniani, hivyo jamii ya Bukoba ijitahidi kuwapatia elimu watoto wao na iwe elimu iliyo bora. Alisema ulimwengo tunauendea sasa ni ulimwengu wa wasomi wa elimu.

“Sisi hapa Tanzania ndio bado tunasubiri ajira baada ya kuhitimu elimu wakati ukienda nchi nyingine mtu kusoma hadi kidato cha sita au chuo kikuu ni kitu cha kawaida na msomi huyo akimaliza shule anauza gazeti au mafenesi na anautumia elimu aliyoipata kutafuta masoko ya biashara yake.

“Tuwatafutie watoto elimu iliyo bora inayoweza kuwasaidia kujiajiri ili wasirudi na vyeti nyumbani na kuanza kulia kuwa wamekosa ajira wakati huo wazazi nao wakilia wamefirisika baada ya kulipa ada,” amesema.

Shekhe Kichwabuta alisema jamii inatakiwa kubadirisha mfumo wa elimu uliopo sasa ambao unasababisha mzazi kulia kuwa mtoto amemfirisi kwa kuwekeza fedha zote kwenye kumlipia ada lakini mtoto huyo anarudi nyumbani na vyeti akilia kuwa amekosa ajira na kukaa nyumbani akiendelea kumtegemea mzazi amtunze.

“Tuwapeleke watoto katika shule ambazo akimaliza na kurudi nyumbani anakuja na kitu ambacho kinaweza kumsaidia kumuingizia kipato wakati akisubiria ajira au kujiajiri ili tusije tukalia wote. Lakini pia wazazi mnatakiwa mchangamkia fursa katika vyuo vya ufundi vinavyojengwa na serikali kwani vitawasaidia vijana wetu kuwajengea uwezo wa kujitegemea baada ya kupata elimu,” alisema Shekhe Kichwabuta.

Naye, Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Kagera, Keffa Elias alisema ili kuondoa utegemezi kwa wanafunzi wanaohitimu masomo yao, serikali imeongeza nguvu kwenye ujenzi wa vyuo vya kati na ufundi ili kuwajengea uwezo wahitimu hao ili waweze kujiajiri au kuajiliwa endapo watashindwa kuendelea na masomo ya sekondari au chuo kikuu.

 “Kupitia vyuo hivyo wahitimu hao wataandaliwa kuwa wataalam wa baadae na kwa Mkoa wa Kagera tumepata fursa ya kujengewa chuo kikubwa cha ufundi stadi (VETA) kilichopo Halmashauri ya Bukoba ambacho tunatarajia kitabeba wanafunzi wengi na kupunguza tatizo la utegemezi kwa vijana kwa kuwajengea uwezo wa kujitegemea na kujiajiri,” alisema Keffa.

Wakati huo Meneja wa shule za Kaizilege na Kemibos, Eurogius Katiti alisema wamefanya maandalizi ya kutosha ya kuhakikisha wahitimu hao wanapeperusha bendera ya shule hiyo katika nafasi za kumi bora kitaifa katika mkutano wa kidato cha sita unaotarajia kuanza Mei mwaka huu.

“Mbali na kuwaandaa kikamilifu wahitimu hawa kwa ajili ya kuchukua nafasi za juu kitaifa lakini pia shule zetu (Kaizilege na Kemebos) zimeanza maandalizi ya kujenga chuo kitakachowawezesha wanafunzi wake kupata ujuzi wa kujiari baada ya kuhitimu masomo yao ya sekondari,” alisema Katiti. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles