23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Wawili wauawa na tembo

NA AMON MTEGA Na Ashura Kazinja

SONGEA/ Morogoro

WATU wawili wamefariki dunia kwa kushambuliwa na tembo katika matukio mawili tofauti.

Katika tukio la kwanza, Rajabu Wewe (43) mkazi wa Kijiji cha Angalia Kata ya Mtina Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, alifariki dunia kwa kukanyagwa na tembo shambani kwake wakati akilinda mazao yake yasiharibiwe na wanyama hao.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Simon Maigwa, alisema tukio hilo lilitokea Aprili 27 saa moja na nusu.

Alisema Weje alipatwa na mkasa huo alipokuwa akilinda mazao yake yasiliwe na wanyama ambapo gafla alitokea tembo na kuanza kumshambulia kwa kumkanyaga sehemu mbalimbali za mwili  hadi kumsababishia kifo.

Maigwa alisema  marehemu katika shamba lake alikuwa akilima mahindi, mpunga, karanga na viazi na kwamba wakati wa mavuno alikuwa akiishi kwenye kibanda alichojenga kwenye shambani hilo.

 Alifafanua mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi na madaktari wa Hospital ya Wilaya ya Tunduru na kukabidhiwa kwa ndugugu zake kwa mazishi.

Katika tukio jingine, mkazi wa Kijiji cha Melela Mlandizi Kata ya Mangae Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro, Romario Matajani  (53) ameuawa kwa kushambuliwa na tembo  majira ya usiku wakati akitoka katika shughuli zake.

Akizungumza na Mtanzania jana shuhuda wa tukio hilo  Kilandi Kileto, alisema wakati wanarudi nyumbani majira ya saa tatu usiku akiwa ameambatana na Matajani,  ghafla likatokea kundi la tembo na kuanza kuwakimbiza.

Alisema taarifa za uwepo wa tembo katika eneo hilo walizipata lakini walijua wameshaondoka kwani imekuwa kawaida ya wanyama hao kukatiza katika makazi ya watu  mara kwa mara.

Amina Said na Alex Wana ambao pia ni wakazi wa kijiji hicho, waliitaka Serikali kuangalia namna ya kuwadhibiti wanyama hao ili kuepusha muingiliano kati yao na  wananachi.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Melela, Ally Nguwa, alisema  changamoto ya uvamizi wa wanyama waharibifu katika eneo hilo ni la muda mrefu na tayari wameshatoa taarifa kwa uongozi wa juu.

Kwa upande wake  Ofisa Wanyamapori Wilaya ya Mvomero, Averina Maklaudi, alisema kwa sasa wameweka kambi katika eneo hilo na wameanza operasheni ya kuwaondoa tembo katika maeneo ya watu huku akitoa wito kwa wananachi kuacha kutembea nyakati za usiku.

Wilaya ya Mvomero imezungukwa na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi ambapo baadhi ya vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo vimekuwa vikivamiwa na tembo mara kwa mara na kuleta athari kwa jamii ikiwemo kuharibu mazao, vifo na majeruhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles