Na MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
WALIMU wawili na mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Chang’ombe, Dar es Salaam wanashikiliwa na polisi kwa kudaiwa kuvujisha mitihani ya kidato cha sita.
Watuhumiwa hao ni Musa Elius (35) ambaye ni mwalimu katika Shule ya Sekondari Chang’ombe, Inocent Mrutu (33), mwalimu mkazi wa Kibamba na Ritha Mosha ambaye ni mtahiniwa wa kidato cha sita.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro, alisema watuhumiwa walikamatwa Mei 5 mwaka huu, baada ya Ofisa wa Baraza la Mitihani (NECTA), Aron Mweteni kutoa taarifa polisi kuhusu uvujaji huo.
Alisema baada ya mwalimu kuingia kwenye chumba cha mtihani na mwanafunzi huyo walikutwa na karatasi yenye maswali na majibu ya somo la Kemia kwa vitendo.
“Baada ya kuwakamata na kuwatilia shaka, ufuatiliaji wa awali ulifanyika kupitia NECTA na kubaini kuwa swali lililokuwapo kwenye karatasi ni miongoni mwa maswali yaliyotoka kwenye mtihani huo,” alisema Sirro.
Jeshi hilo pia linamshikilia mwanafunzi wa Chuo cha St. Joseph, Lewis Mbise (23) kwa a kukutwa na bastola moja na risasi 13.
Mwanafunzi huyo alikamatwa Mei 4 mwaka huu, katika eneo la Mbezi Magari Saba akiwa na risasi 13 ndani ya magazine.
Baada ya kuhojiwa mwanafunzi huyo alikiri kuwa bastola hiyo aliiba nyumbani kwa baba yake mzazi, Lazaro Mbise na Sh 800,000.
Sirro aliamuru mzazi wa mwanafunzi huyo akamatwe na kufikishwa mahakamani kwa kushindwa kuhifadhi vizuri silaha hiyo.