23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Waumini KKKT wamkataa Msaidizi wa Askofu

kanisa
Kanisa

Na Upendo Mosha, Moshi

WAJUMBE wa Mkutano Mkuu wa 33 wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini, wamemkataa Askofu Msaidizi wa jimbo hilo aliyekuwa amependekezwa kugombea nafasi hiyo, Mchungaji Elinganya Saria.

Tukio hilo lilitokea mjini hapa jana baada ya jina la mchungaji huyo kupendekezwa na Halmashauri Kuu ya Dayosisi kwa ajili ya kupigiwa kura.

Wakati wa tukio hilo, jina la Mchungaji Saria ndilo lilikuwa pekee lililokuwa limependekezwa, lakini wajumbe walilikataa licha ya kulipigia kura mara tatu.

Kutokana na hali hiyo, uchaguzi huo ulilazimika kuahirishwa kwa ajili ya kuandaa mkutano mkuu mwingine utakaomchagua Askofu Mkuu Msaidizi.

Awali wajumbe wa mkutano huo uliofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Stephano Moshi, walimchagua Mchungaji Dk. Fredrick Shoo kuwa Askofu Mkuu Mteule wa Dayosisi hiyo kwa kipindi cha miaka 10 ijayo.

Akitangaza matokeo hayo, Askofu Mkuu wa Dayosisi hiyo aliyemaliza muda wake, Dk. Martin  Shao, alisema Dk. Shoo alipata kura 324 kati ya kura 334 zilizopigwa.

Askofu Mkuu Mteule, Dk. Shoo alizaliwa mwaka 1959 na kabla ya uchaguzi huo, alikuwa Msaidizi wa Askofu wa Dayosisi hiyo kwa miaka 10 kuanzia mwaka 2004.

Alibarikiwa kuwa Mchungaji Desemba 14 mwaka 1986 katika Usharika wa Lyamungo Kati. Kuanzia mwaka 1986 hadi 1988, alikuwa Mchungaji Kiongozi katika Usharika wa Mwika.

Alipata shahada ya uzamili na uzamivu nchini Ujerumani. Alikuwa Mkuu wa Chuo cha Biblia Mwika, mwaka 1995 hadi 2003.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles