25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

WAUAJI RUFIJI WAMBIPU IGP SIRRO

ASHA BANI-DAR ES SALAAM



WAUAJI wilayani  Rufiji Mkoa wa Pwani ‘wamembipu’ Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon  Sirro, kwa kuua mtu mwingine usiku wa kuamkia jana katika Kitongoji cha Kazamoyo Kijiji cha Ikwiriri Kaskazini wilayani humo.


Wauaji hao   walivamia  kijijini hapo   na kumpiga risasi shingoni,  Erick Mwarabu (38) ambaye ni  fundi rangi.


Kwa mujibu wa mtoa taarifa,  Mwarabu akiwa nyumbani kwake   saa 8.00 usiku juzi, wauaji hao walifika na kumpiga     risasi   shingoni ambayo ilitokea kichwani upande wa kulia   kati  ya jicho na sikio na akafariki dunia papo hapo.


  Mkuu wa  Wilaya ya Rufiji,  Juma Njwayo, aliithibitishia MTANZANIA  kwa  simu kwamba tukio hilo la mauaji lilitokea usiku wa kuamkia jana.


Alisema   tayari mwili wa marehemu umekwisha kufanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa kwa ndugu zake  kwa mazishi.
Kifo cha Mwarabu kinafanya   idadi ya watu waliouawa   hadi sasa katika wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji mkoani Pwani kufikia 30.
Kutokana na vitendo hivyo vya mauaji, hivi karibuni IGP Sirro, alitangaza mkakati wake ikiwamo jinsi ya kukomesha mauaji katika maeneo hayo.


  IGP Sirro aliapa kupambana na wauaji hao huku akiahidi donge nono la   Sh milioni 10 kwa yeyote atakayetoa taarifa za kuwezesha kukamatwa wauaji hao.
Alisema polisi  wanaendelea na operesheni mbalimbali  kuhakikisha  vitendo hivyo haviendelei na kwamba lazima watafanikiwa kubaini mzizi wa mauaji hayo.


Mei 21  mwaka huu, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, alitembelea eneo hilo na kuteta na askari wa operesheni maalumu ya kuwasaka wauaji wilayani Kibiti. 


Alisema  mauaji hayo sasa yametosha akisisitiza  Serikali haitakuwa tayari kuona vitendo hivyo vikiendelea kama ilivyo  Somalia.
Ziara hiyo ya ghafla ya Waziri Nchemba ilitokana na   mauaji ya mara kwa mara ya raia  ambayo yamekuwa yakifanywa na watu wasiojulikana.


Akizungumza baada ya kuwatembelea   polisi  katika kambi maalumu ya operesheni ya kusaka wahalifu katika Kata ya Bungu, alisema  Serikali  imejipanga kukomesha hali hiyo kwa sababu kufuga wauaji na wahalifu kuna gharama.
“Tunaendelea kufuatilia kazi   mnayoendelea kufanya,   tuendelee kusonga mbele. Nikiziangalia takwimu na mwenendo, nazidi kupata maswali na naendelea kuona kuwa kuna kamchezo kanachezwa. 


“Mauaji haya waliyoyafanya inatosha. Lazima tuwatie nguvuni, hatuwezi kuruhusu jambo hili likaendelea na kamchezo haka kakaendelea.


“Anayefanya mauaji haya, anayeshirikiana na anayeshangilia hiki kinachofanyika wote tunawaweka katika kundi moja. Kufuga wauaji na wahalifu kuna gharama,”alisema.
Nchemba  aliwataka polisi hao kukaa kimkamkati kuwakamata wauaji hao.


Alisema ni muhimu polisi waondokane na dhana kwamba wametokomea kusikojulika bali wawakamate.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles