Jonas Mushi na Ruth Mnkeni, Dar es salaam
JESHI la Polisi limewakamata watumishi 12 wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwachunguza kuhusu wizi na utoroshaji wa makontena 329 katika bandari ya Dar es Salaam.
Saba kati yao wanatoka TRA ambao walisimamishwa kazi na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Wengine wanatoka taasisi nyingine za serikali ambazo polisi hawakutaka kuzitaja hadi wakamilishe uchunguzi dhidi yao.
Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Diwani Athumani alisema jana kuwa idadi hiyo inajumuisha watuhumiwa watano wanaotoka TRA na Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA).
Diwani aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Kamishna wa Idara ya Forodha na Ushuru wa TRA, Tiagi Masamaki (56) na Meneja Kitengo cha Huduma za Ushuru TRA, Habib Mponezya (45).
Wengine ni Msimamizi Mkuu Kitengo cha Ushuru wa Forodha (ICD) AZAM, Eliach Mrema (31), Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Kompyuta (TEHAMA)-TRA, Haroun Mpande (27) na Mchambuzi Mwandamizi wa Masuala ya Biashara, Hamis Omary (48).
“Kama mnakumbuka Novemba 27 mwaka huu Waziri Mkuu Majaliwa alifanya ziara ya kushtukiza katika bandari ya Dar es Salaam.
“Pamoja na mambo mengine alieleza wizi wa makontena 349 ya bidhaa mbalimbali.
“Kutokana na wizi huo aliagiza polisi kufanya uchunguzi na kuwakamata wahusika wote waliojihusisha na wizi huo,” alisema Athumani.
Kuhusu watuhumiwa wengine saba waliokamatwa ambao si watumishi wa TRA alisema majina yao hayatatajwa kwa sasa kutokana na sababu za upelelezi.
Alisema uchunguzi dhidi yao unatarajiwa kukamilika mapema iwezekanavyo na kuwafikisha watuhumiwa hao mahakamani.
Aliwataka wote wanaojijua kuhusika kwa namna moja au nyingine katika wizi huo kujisalimisha wenyewe.
“Uchunguzi unaendela kuwabaini watuhumiwa wengine na nitumie nafasi hii kutoa rai kwa yeyote anayejijua kuhusika kwa namna moja au nyingine ajisalimishe kwa vile alipo tutamfikia,” alisema Athumani.
Alisema uchunguzi huo unafanywa na wataalamu wa jeshi hilo waliobobea katika uchunguzi wa makosa ya uhalifu wa fedha.