24.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Watuhumiwa wawili Nida wadhaminiwa

MAIMU

AZIZA MASOUD NA PAULINA KEBAKI – DAR ES SALAAM

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jana imewaachia kwa dhamana washtakiwa wawili kati ya wanane ambao juzi walisomewa mashtaka 27 ya uhujumu uchumi na kuisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 1.6.

Watuhumiwa hao, Avelin Momburi na Joseph Makani, ni miongoni mwa waliokuwa wafanyakazi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida). Momburi alikuwa Meneja Biashara na Makani alikuwa Mkurugenzi wa Teknolojia wa Habari na Mawasiliano (Tehama).

Wote wawili walitakiwa kutimiza masharti ya dhamana kwa kuwa na wadhamini wawili wawili walioweka bondi hati za nyumba zenye thamani ya Sh milioni 200.

Mbali na bondi hiyo, wadhamini walipaswa kukidhi vigezo vya kuwa na barua kutoka serikalini ama taasisi inayotambulika.

Dhamana hiyo pia imewaelekeza washtakiwa kutotoka nje ya Mkoa wa Dar es Salaam bila kibali maalumu cha Mahakama.

Momburi na Makani walipewa dhamana baada ya makosa yao kuwa na thamani isiyozidi Sh milioni 10 na kwamba hayapo kwenye orodha ya makosa ya uhujumu uchumi.

Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo juzi  mbele ya Hakimu Mkazi, Respicious Mwijage, wakikabiliwa na mashtaka ya kutumia madaraka  yao vibaya, kula njama, kutumia nyaraka za uongo kumdanganya mwajiri na kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya Sh 1,169,352,931.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Awamu Mbagwa, akishirikiana na mawakili kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Janeth Machulya, Leonard Swai, Joseph Kiula na Fatuma Waziri, waliwasomea washtakiwa hao mashtaka yanayowakabili.

Mshtakiwa Momburi na wenzake wawili wanadaiwa kati ya Februari 22 na Aprili 17, 2012 katika ofisi za makao makuu ya Nida walitumia madaraka yao vibaya kwa kupitisha malipo ya Sh 22,582,281 kwa Kampuni ya Aste Insurance Brokers hivyo kuifanya kampuni hiyo kupata faida ya kiasi hicho.

Katika mashtaka mengine, Makani na wenzake wanadaiwa kati ya Januari 29 na 30, 2013 katika makao makuu hayo walitumia madaraka yao vibaya kuidhinisha malipo ya Dola za Marekani milioni mbili kwa IRIS Corporation Berhad.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles